IQNA

Wamisri waandamana kupinga picha zinazomvunjia heshima Mtume wa Uislamu

17:03 - November 12, 2011
Habari ID: 2221206
Mamia ya wananchi wa Misri wameandamana mbele ya ubalozi wa Ufaransa mjini Cairo wakipinga hatua ya gazeti la Charlie Hebdo ya kuchapicha picha zinazomvunjia heshima Mtume Muhammad (saw).
Khalid Said ambaye ni miongoni mwa watayarishaji wa maandamano hayo amesema kuwa maandamano hayo yamefanyika kupinga msimamo rasmi wa serikali ya Ufaransa ambayo inakutambua kuvunjiwa heshima Mtume wa Uislamu kuwa ni uhuru wa kusema na kujieleza.
Khalid Said ameongeza kuwa Waislamu wa Misri wataanza kususia bidhaa za Ufaransa kutokana na msimamo wa serikali ya Paris wa kuunga mkono picha hizo zinazovunjia heshima matukufu ya Kiislamu.
Ni vyema kukumbusha hapa kuwa gazeti la kila wiki la Charlie Hebdo na lile la Liberation yanayochapishwa nchini Ufaransa wiki iliyopita yalichapisha picha zinazomdhalilisha na kumvunjia heshima Mtume Muhammad (saw) kwa kisingizio cha uhuru wa kujieleza. Kitendo hicho kimewakasirisha mno Waislamu wa Ufaransa na maeneo mbalimbali duniani. 897152

captcha