IQNA

Rais Ahmadinejad akutana na Waziri wa Ulinzi wa Zimbabwe

11:13 - March 15, 2012
Habari ID: 2292118
Rais Mahmoud Ahmadinejad wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuna haja ya kuimarisha mapambano dhidi ya mashinikizo na vikwazo vya maadui.
Rais Ahmadinejad ameyasema hayo katika mazungumzo yake na Waziri wa Ulinzi wa Zimbabwe Emmerson Dambudzo Mnangagwa aliyekuwa safarini hapa nchini. Ameongeza kuwa vikwazo vinapaswa kubadilishwa kuwa fursa ya ustawi na maendeleo.
Aidha amesema kuwa Iran na Zimbabwe daima zitasimama pamoja katika uga wa kimataifa kwani nchi hizi mbili ziko katika mkondo mmoja na zinachukua hatua za kustawisha thamani za kibinaadamu kwa maslahi yao ya kitaifa.
Rais wa Iran amesema msimamo kama huo bila shaka utapelekea kupatikana ushindi. Rais Ahmadinejad amesisitiza kuwa Iran iko tayari kuimarisha uhusiano wa pande zote na Zimbabwe. Naye Waziri wa Ulinzi wa Zimbabwe Emmerson Dambudzo Mnangagwa amesema sawa na Iran, taifa la Zimbabwe litakabiliana na mashinizio ya kigeni na kugeuza vikwazo kuwa fursa kwa maslahi ya kitaifa.
Katika safari yake nchini Iran iliyomalizika Jumanne, Waziri wa Ulinzi wa Zimbabwe na mwenzake wa Iran Brigedia Jenerali Ahmad Vahidi walitia saini hati za ushirikiano wa nchi mbili katika sekta ya ulinzi.
971751
captcha