IQNA

Waislamu Kenya waeleza wasiwasi wao kuhusu muswada wa kupambana na ugaidi

17:25 - July 10, 2012
Habari ID: 2365435
Jumuiya mbalimbali za Kiislamu nchini Kenya zimeelezea wasiwasi wao kutokana na muswada wa sheria ya kupambana na ugaidi iliyopendekezwa na serikali kwenye bunge la nchi hiyo.
Jumuiya hizo za Kiislamu zinasema kuwa kupasishwa kwa muuswada huo ni sawa na kupasisha mapambano dhidi ya Uislamu.
Mgombea ugavana wa mji wa Mombasa Sulaiman Shahbal amesema muswada wa kupambana na ugaidi uliopendekezwa bungeni unakiuka uhuru wa wananchi wa Kenya na unawalenga Waislamu waliowachache nchini humo. Amesema Waislamu hawapingi harakati za kupambana na ugaidi lakini miswada kama hiyo inapaswa kuheshimu haki za raia Waislamu.
Shahbal amesisitiza kuwa miswada inayopendekezwa bungeni kwa jina la kupambana na ugaidi nchini Kenya huwa na maana ya miswada ya kupambana na Waislamu kwa sababu Waislamu wanatambuliwa kuwa ni magaidi nchini humo.
Viongozi wengi wa Kiislamu nchini Kenya wameelezea wasiwasi wao kuhusu muswada huo wa kupambana na ugaidi ambao pia umekosolewa na taasisi na jumuiya nyingi za Kiislamu.
Waislamu wametaka muswada huo uwekwe wazi kabla ya kufikishwa bungeni ili kila Mkenya ajue vipengee vyake. 1049607
captcha