Katibu Mkuu wa harakati ya Hizbullah ya Lebanon Sayyid Hassan Nasrullah jana usiku alihutubia umati mkubwa wa watu mjini Beirut kwa mnasaba wa kukumbuka ushindi wa harakati hiyo katika vita vya siku 33 dhidi ya utawala ghasibu wa Israel miaka sita iliyopita na kueleza kwa undani yaliyojiri katika vita hivyo na hali ya sasa ya kieneo na kimataifa.
Sayyid Nasrullah amesisitiza katika hadhara hiyo ya maelfu ya Walebanon na shakhsia wa kimataifa kwamba Wazayuni wa Israel wamekiri kwamba walishindwa katika vita vya siku 33 dhidi ya Lebanon na wangali wanasumbuliwa na kiwewe cha kushidwa katika vita hivyo.
Katibu Mkuu wa Hizbullah amesisitiza kuwa nguvu ya harakati hiyo imeongezeka kwa kiwango kikubwa tangu baada ya vita vya siku 33 na kwamba harakati hiyo iko tayari kwa mashambulizi ya aina yoyote ile ya Israel.
Ameashiria njama zinazofanywa na maadui dhidi ya nchi za Mashariki ya Kati na kusema baada ya vita vya siku 33 dhidi ya Lebanon maadui walianza awamu mpya ya kutaka kuiondoa madarakani serikali ya Rais Bashar Assad wa Syria na kuiweka nchi hiyo katika ajenda ya Marekani na Israel.
Amelaani mauaji ya kigaidi yaliyotokea jana mjini Damascus na kusisitiza kuwa Hizbullah itaendelea kuiunga mkono Syria ambayo imekuwa nguzo muhimu ya wapigania uhuru wa Palestina na wanamapambano wa Lebanon. 1057102