Ali Larijani aliyasema hayo jana jioni mwishoni mwa kongamano la kimataifa la 28 la Umoja wa Kiislamu lililofanyika mjini hapa Tehran ambapo sanjari na kuashiria nukta tofauti kuhusiana na umoja wa Waislamu na tishio linaloukabili umoja huo, alisema kuwa, kongamano hilo lilikuwa ni fursa bora kwa ajili ya maulama na wanasiasa wa Kiislamu ili waweze kuandaa mikakati katika kutatua matatuzi yanayoukabili ulimwengu wa Kiislamu. Spika wa Majlisi ya Ushauri wa Kiislamu ya Iran ameongeza kuwa, kwa miongo kadhaa sasa kumeonekana nafasi na ongezeko kubwa la maendeleo katika nchi za Kiislamu, ikiwemo ongezeko la vyuo vikuu na kwamba nchi kama Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Malaysia, Indonesia na Pakistan zimeweza kuinuka kielimu kwa kupatikana wataalamu na wanafikra wakubwa katika nchi hizo. Ametaka kuandaliwe mazingira yatakayosaidia kuboresha hali ya sasa ya Waislamu duniani. Aidha amesema kuwa, ujumbe na harakati za Imam Khomein, Mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, zilikuwa ni kwa maslahi ya Uislamu. Akiashiria tishio la makundi ya kigaidi na kitakfiri dhidi ya ulimwengu wa Kiislamu amesema, ripoti za kipelelezi zinaonyesha kuwepo mafungamano ya karibu mno kati ya makundi hayo na vyombo vya kijasusi vya Magharibi katika kufanya mauaji na kueneza fitina ndani ya nchi za Kiislamu na katika eneo la Mashariki ya Kati.../mh