Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, vikosi vya usalama Saudia vimefunga msikiti huo wa Mashia na kuzuia sala ya Ijumaa kusaliwa hapo.
Kwingineko vikosi vya usalama Saudia katika eneo hilo la Al Ahsa, vimemfunga kifungo cha nyumbani Sheikh Hussein al-Radhi, kama njia mojawapo ya kumzuia kutoa hotuba zilizo dhidi ya utawala wa kidikteta wa nchi hiyo ambao haupendi kukosolewa kwa njia yoyote ile.
Hivi karibuni Sheikh al-Radhi alikosoa kitendo cha kuuliwa shahidi Sheikh Nimr Baqir al-Nimr, mwanachuoni na mwanamapambano mkubwa wa Waislamu wa Kishia aliyeuawa kidhalimu kwa kukatwa shingo na maafisa wa Saudia, na kusema utawala huo hauko tayari kukosolewa kutokana na kutojiamini. Amesema kwa msingi huo utawala huo humuua kila mpinzani au mkosoaji anayeamua kuukosoa. Matamshi hayo yamewafanya maafisa usalama wa Saudia kumzuilia kifungo cha nyumbani Sheikh Hussein al-Radhi, suala ambalo limelaaniwa na wanaharakati wa haki za binaadamu nchini humo. Weledi wa mambo wanaamini kuwa, siasa za utumiaji mabavu zinazofuatwa na utawala wa Aal Saud dhidi ya Waislamu wa madhehebu ya Shia, zitaifanya hali ya mambo katika eneo la mashariki mwa nchi hiyo, kuwa mbaya zaidi.