IQNA

Utawala wa Bahrain walaaniwa vikali baada ya kuwanyonga vijana kwa tuhuma hewa

16:02 - July 28, 2019
Habari ID: 3472061
TEHRAN (IQNA) - Utawala wa kiimla wa ukoo wa Aal Khalifa nchini Bahrian umelaanivwa vikali baada ya kuwanyonga vijana wawili raia wa nchi hiyo kwa tuhuma zisizo na msingi za kumuua afisa wa wizara ya mambo ya ndani mwaka 2017.

Ahmad Issa al-Mullali, 24, na Ali Hakim al-Arab, 25, walinyongwa Jumamosi katika Jela ya Jaw prison, kusini mwa mji mkuu wa Bahrain, Manama, baada ya mkutano na familia zao.
Wapinzani nchini Bahrain katika Jumuiya ya kitaifa na Kiislamu ya Al-Wifaq, wametoa wito kwa wananchi kufanya maandamano ya kulaani na kulalamikia jinai ya utawala wa Aal Khalifa wa kuwanyonga vijana wawili kwa tuhuma hewa.
Jumuiya ya Al- Wifaq imethibitishwa kuwa, vijana wawili raia wa nchi hiyo wamenyongwa mapmea na utawala dhalimu wa Aal- Khalifa kwa tuhuma za kumuua afisa wa wizara ya mambo ya ndani mwaka 2017.
Utawala wa kiimla wa Aal-Khalifa umewanyonga vijana hao licha ya mashirika ya kutetea haki za binadamu yakiwemo ya Amnesty International na Human Rights Watch pamoja na Umoja wa Mataifa kutoa miito hapo jana ya kutaka kusimamishwa utekelezaji wa adhabu hiyo ya kifo.
Shirika la Human Rights Watch limesema, mahakama za Bahrain haziko huru na zinatoa hukumu kiuonevu na kubainisha kuwa, mahakama hizo ndio mkandamizaji mkuu wa raia kwa kutoa hukumu za kidhalimu na kiuonevu kwa watu wanaoandamana kwa amani.
Tangu Februari mwaka 2011, wakati ulipoanza mwamko wa Kiisamu Asia Magharibi, Bahrain imekuwa uwanja wa maandamano ya amani ya wananchi wanaopinga utawala wa kifalme wa ukoo wa Aal Khalifa.
Wananchi hao wanataka kuwepo uhuru, utekelezwe uadilifu, ukomeshwe ubaguzi na kuundwa serikali itakayochaguliwa na wananchi wenyewe.
Hata hivyo kwa msaada wa wanajeshi wa Saudi Arabia na askari usalama wa Imarati waliotumwa nchini Bahrain kupitia mpango wa ulinzi wa Ngao ya Kisiwa, utawala wa Aal Khalifa unatumia mkono wa chuma kukabiliana na matakwa ya wananchi hao.
Kwa mujibu wa duru za haki za binadamu, Bahrain ina idadi kubwa zaidi ya wafungwa wa kisiasa kulinganisha na idadi ya watu katika nchi hiyo ndogo zaidi katika Ghuba ya Uajemi.

3469049

captcha