IQNA

Bunge la Iraq laendeleza mazungumzo kuhusu kuondoka askari vamizi wa Marekani

17:55 - February 04, 2020
Habari ID: 3472440
TEHRAN (IQNA) – Mkakati wa kutaka wanajeshi vamizi wa Marekani waondoke Iraq unaendelea kushika kasi nchini humo.

Katika tukio la hivi karibuni, Muungano wa 'Sairoon' katika bunge la Iraq umeitisha kikao kikuu cha kitaifa kwa ajili ya kuchunguza mpango wa kuwatimua askari wa Marekani kutoka katika ardhi ya nchi hiyo.

Alau al-Rabii, mmoja wa viongozi wa muungano huo ameyasema hayo leo mjini Baghdad ambapo sambamba na kubainisha kuwa kuendelea kuwepo askari wa Kimarekani nchini Iraq ni tishio kwa usalama na uthabiti wa nchi hiyo, ameongeza kuwa makundi, vyama, makabila na dini zote lazima zichukue uamuzi wa jumla kwa ajili ya kuwatimua askari hao wa Kimarekani kutoka nchi hiyo. Naye Karim Al-Muhammadawi, mjumbe wa kamisheni ya usalama na ulinzi nchini Iraq ameashiria kuwepo mashinikizo ya serikali ya Washington kwa Baghdad ya kuitaka nchi hiyo kusitisha uamuzi wa bunge la Iraq wa kuwatimua askari hao vamizi na badala yake waendelee kubakia katika kambi ya kistratijia ya Ain Al Assad.

Itakumbukwa kuwa baada ya Marekani kutekeleza shambulizi la kigaidi dhidi ya Luteni Jenerali Qassem Soleimani, Aliyekuwa Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran IRGC pamoja na Abu Mahdi al-Muhandis, Naibu Mkuu wa Harakati ya Wananchi ya Hashdu sh-Sha'abi ya Iraq hapo tarehe 3 ya Januari mwaka huu, tarehe tano ya mwezi huo wawakilishi wa wananchi katika bunge la nchi hiyo walipitisha mpango wa kuwatimua askari wa Kimarekani katika ardhi ya Iraq. Mbali na hayo viongozi wengine wengi wa ngazi za juu wa Iraq wamekuwa wakisisitiza udharura wa kuondoka askari hao wa Marekani katika ardhi ya nchi hiyo.

3876389

captcha