IQNA

Kiongozi Muadhamu amuomboleza Ayatullah Taskhiri, asema ametoa huduma kwa Ulimwengu wa Kiislamu

21:52 - August 18, 2020
Habari ID: 3473079
TEHRAN (IQNA) - Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Ali Khamenei ametuma salamu za rambirambi kwa mnasaba wa kuaga dunia mwanazuoni, mujahid na mtetezi wa Uislamu, Hujjatul Islam Walmuslimin Muhammad Ali Taskhiri aliyekuwa kiongozi wa Baraza Kuu la Jumuiya ya Kimataifa ya Kukurubisha Pamoja Madhehebu ya Kiislamu na Mshauri wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika Masuala ya Ulimwengu wa Kiislamu.

Katika ujumbe wake wa salamu za rambirambi, Ayatullah Khamenei amewapa mkono wa pole watu wa familia ya marehemu Hujjatul Islam Walmuslimin Taskhiri, jamaa zake, washirika na marafiki zake na kusema: Shakhsia huyu aliyechapa kazi bila ya kuchoka na kutoa huduma kubwa katika jumuiya mbalimbali za kimataifa za Kiislamu, ameacha faili linalong'aa. 

Ayatullah Khamenei amemuombea maghufura na rehma za Mwenyezi Mungu marehemu Taskhiri na kusema: Azma yake kubwa na moyo wa kujituma uliomuwezesha kushinda hata maradhi ya kimwili kwa miaka kadhaa, na vilevile huduma zake kubwa na zilizojaa baraka katika maeneo mbalimbali, vinaonekana waziwazi.

Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pia ametoa salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Hujjatul Islam Muhammad Ali Taskhiri aliyekuwa kiongozi wa Baraza Kuu la Jumuiya ya Kimataifa ya Kukurubisha Pamoja Madhehebu ya Kiislamu na Mshauri wa Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu katika Masuala ya Ulimwengu wa Kiislamu.

Rais Rouhani amesema: Hujjatul Islam Walmuslimin Taskhiri ambaye alikuwa kinara wa kuhubiri umoja na mshikamano wa Umma wa Kiislamu na mhubiri mkubwa wa mafundisho na utamaduni wa Ahlibaiti wa Mtume Muhammad (saw), ametumia sehemu kubwa ya umri wake kwa ajili ya kulingania maarifa ya dini ya Uislamu na kukurubisha pamoja madhehebu za Kiislamu, na amebakisha nyuma faili linalong'aa na kumeremeta.

Hujjatul Islam Walmuslimin Muhammad Ali Taskhiri ameaga dunia mapema leo katika mojawapo ya hospitali za Tehran kutokana na matatizo ya moyo.

Sheikh Taskhiri ambaye amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 76 ni miongoni mwa wanazuoni mashuhuri wa Kiislamu waliotoa huduma kubwa za kulingania dini hiyo na kujenga maelewano, umoja na mshikamano baina ya wafuasi wa madhehebu mbalimbali za Waislamu.

Shekh Ali Taskhiri ameandika makumi ya vitabu na makala mbalimbali kuhusu maudhui tofauti.  

3917395

captcha