Dk Mohammad Javad Zarif amesema hayo katika ujumbe alioutuma usiku wa kuamkia leo kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter na kuongeza kuwa, Iran inawaita wote katika mazungumzo. Pia ameandika kwa lugha ya Kiarabu maneno yenye maana isemayo: Mazungumzo ndiyo njia pekee ya kukomesha hitilafu na wasiwasi.
Ameashiria pia jinsi alivyobwagwa Donald Trump katika uchaguzi wa rais nchini Marekani na kusisitiza kuwa, Trump ameenda lakini sisi tumebakia na majirani zetu.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran vile vile amesema, usalama haupatikani kwa kuwategemea watu baki, bali jambo hilo linapoteza kabisa matumaini.
Katika kipindi cha miaka minne ya urais wake huko Marekani na kwa kushirikiana na utawala wa Kizayuni wa Israel na baadhi ya vibaraka wa nchi za Kiarabu, Donald Trump alianzisha muungano ulio dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran lakini alishindwa.
Iran muda wote imekuwa ikisisitiza kwamba mazungumzo, kuheshimiana na kuishi pamoja kwa amani nchi za eneo hili ndiyo stratijia yake kuu na mara zote imekuwa ikitangaza hamu yake ya kuwa na uhusiano wa kimantiki, mzuri na wa kuheshimiana na majirani zake wote.