Daktari Saeed Namaki, Waziri wa Afya wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amezungumza kuhusu chanjo hiyo ya Iran kufanyiwa majaribio kwa mwanadamu na kusema: "Leo ni kati ya siku zenye matumaini zaidi kwa taifa la Iran. Kufuatia jitihada za wasomi na wataalamu wa Iran kuhusu COVID-19, tumepita awamu ya utafiti na sasa tumeweza kumdunga mwandamu chanjo hii."
Chanjo hiyo ambayo inajulikana kama COVIRAN Barekat imetegenezwa katika Idara ya Utafiti ya Taasisi ya Utekelezaji wa Maagizo ya Imam Khomeini (MA).
Tayyibah Mokhberi bintiye mkurugenzi wa Tume ya Utekelezaji wa Maagizo ya Imam Khomeini MA alikuwa mtu wa kwanza kujitolea kudungwa chanjo hiyo ya Iran.
Naibu Waziri wa Afya na Mafunzo ya Tiba wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, hadi hivi sasa hakuna athari zozote hasi zilizooneshwa na watu waliofanyiwa majaribio hayo, licha ya kupita zaidi ya masaa 24 ya tangu kudungwa chanjo hiyo.
Daktari Ali Reza Raisi amesema hayo Jumatano na huku akielezea umuhimu wa radiamali za watu wanaofanyiwa majaribio ya chanjo hiyo ya corona ya Iran kabla ya kuzalishwa kwa wingi amesema kuwa, majaribio mengine yatafanyika katika kipindi cha siku 14 zijazo.
Naibu Waziri wa Afya wa Iran pia amesema, awamu ya tatu ya majaribio ya chanjo hiyo ya corona ya Iran itafanyika baada ya siku 28 na kama katika hatua zote hizo itapasi, basi itaanza kuzalishwa kwa wingi hivi karibuni. Dk Raisi vile vile amesema, Iran ina uzoefu na teknolojia kubwa katika uzalishaji wa chanjo, na wasomi na wanasayansi wa Iran wanajiamini katika uwanja huo.
Vikwazo vya kidhalimu
Janga la COVID-19 ni janga la kimataifa. Ugumu wa kukabiliana na janga la corona Iran umebainika zaidi kutokana na vikwazo vya kidhalimu vya Marekani dhidi ya nchi hii.
Katika uga huo, Marekani imekuwa ikifanya juu chini kuhakikisha kuwa Iran haipati dawa na vifaa vya kitiba kwa ajili ya kuwatibu wagonjwa wa corona. Hata baada ya Iran kutangaza kuwa tayari kununua chanjo ya homa kali ya influenza ambayo huenea zaidi wakati wa msimu huu wa baridi nchini, Marekani ilihakikisha kuwa imeweka vizingiti ili Iran isipate kununua chanjo hiyo.
Maadui wa taifa la Iran huwa wanatumia kila mbinu kulipa pigo taifa la Iran. Serikali nyingi duniani zimekabiliwa na mtihani mkubwa kuhusu namna ya kukabiliana na kirusi cha corona. Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imeonyesha kuwa haiwezi kusalimu amri mbele ya matatizo na vikwazo vya maadui.
Katika kuhakikisha kuwa wananchi wake wanapata chanjo ya corona, Iran imekuwa ikifuatilia njia tatu.
Njia ya kwanza ni kupitia kununua katika soko la kimataifa chanjo ambazo zimeainishwa katika mpango maalumu wa Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa ajili ya nchi zote za dunia. Hadi sasa chanjo za mashirika kadhaa zimeanza kutumiwa. Chanjo ya Oxford/AstraZeneca na Moderna ni chanjo ambazo zimeidhinishwa na WHO. Iran imeagiza dozi milioni 16 na laki nane za chanjo hizo kwa ajili ya watu milioni nane na laki nne ambao wako katika makundi yenye hitajioo la kimsingi la chanjo. Kila mgonjwa hupata dozi mbili za chanjo hiyo.
Njia ya pili ambayo Iran inatumia kupata chanjo ni kutegemea vyanzo vingine huru vya kimataifa na hadi sasa mazungumzo yanaendelea kuhusiana na hilo.
Njia ya tatu ambayo Iran imekuwa ikifuatilia katika kupata chanjo, ni ushirikiano katika uzalishaji chanjo.
Ikumbukwe kuwa Iran ina uzoefu wa karibu miaka 100 katika uzalishaji wa chanjo katika Taasisi ya Pasteur ya Iran na imekuwa ikiuza chanjo zilizotegenezwa ndani ya nchi katika maeneo mengine duniani.
Katika kukabiliana na COVID-19, lengo kuu la wanasayansi na wasomi wa Iran limekuwa ni kuzalisha chanjo ndani ya nchi. Kuhusiana na hilo, Iran imetumia uwezo wake wote wa kitaifa pamoja na irada imara katika kukabiliana na janga la COVID-19 na kulibadilisha tishio la janga hilo kuwa fursa. Hivi sasa jitihada za Iran zimezaa matunda na utengenezaji wa chanjo ya corona ya Iran umefika katika kiwango cha majaribio kwa wanadamu na hatimaye kuzalishwa kwa wingi. Utegenezaji wa chanjo hiyo ya Iran unafanyikwa kwa uangalizi wa Shirika la Afya Duniani.
Inatazamiwa kuwa, kufuatia kuanza majaribio ya chanjo hiyo kwa mwanadamu, ifikapo mwaka mpya wa Kiirani wa 1400 Hijria Shamsia, ambao utaanza Machi 21, Iran itakuwa moja kati ya wazalishaji wakubwa wa chanjo ya COVID-19 katika eneo na hivyo itaweza kukidhi mahitaji yake katika uga huo.