Mkuu wa Halmashauri ya Kuainisha Maslahi ya Mfumo wa Kiislamu amesema kuhusiana na mazungumzo ya nyuklia kati ya Iran na mataifa sita yenye nguvu duniani kwamba, mazungumzo hayo yanaweza kutatua masuala yote kama nchi za Magharibi zitaacha kutoa visingizio.

Kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la Habari za Qur'ani IQNA, Ayatullah Ali Akbar Hashemi ameyasema hayo mbele ya hadhara ya wanachuo wa vyuo vikuu mbalimbali kote nchini, Rafsanjani ameongeza kuwa, nchi za Magharibi zinapaswa kujiepusha na vitimbi vya Wazayuni na kusisitiza kwamba wananchi wa Iran ni watu wenye uelewa na wala hawazungumzi kwa kutumia lugha ya vitisho. Ayatullah Rafsanjani amebainisha kuwa, wananchi wa Iran wanataka kustafidi na teknolojia ya nyuklia yenye malengo ya amani kwa kuwatumia wataalamu wake wa ndani. Akizielezea njama za madola ya kikoloni na kibeberu za kuyarudisha nyuma kimaendeleo baadhi ya mataifa mengine, Ayatullah Rafsanjani amesema kuwa, vitendo vya kushadidishwa taasubi za kimadhehebu na kuwauwa watu wasio na hatia haviendani na sheria, utamaduni wala ustaarabu wa Kiislamu.