Sheikh Hussein al Bayat, mwanazuoni mashuhuri wa mji wa Qatif huko Saudia amesema kuwa kimya cha Waislamu katika baadhi ya nchi za Kiarabu na Kiislamu na kutofanya kwao shughuli za maombolezo ya kukumbuka mauaji na harakati ya Imam Hussein, mjukuu wa Mtume Muhammad (saw) ni jambo ambalo halikubaliki, kwani harakati ya Ashura ni tukio adhimu lililotikisa umma mzima wa Kiislamu.
Sheikh Bayat ambaye alikuwa akizungumza katika Msikiti wa Rasurul Aadham mjini Qatif huko Saudi Arabia amewataka Waislamu wa nchi mbalimbali kama Sudan, Morocco, Tunisia, Kuwait, Misri na kwengineko kutilia maanani tukio la Ashura na harakati ya Imam Hussein (as). Amesema Hussein (as) ni mjukuu wa Mtume Mtukufu ambaye aliuawa shahidi kwa sababu ya kutetea dini tukufu ya Kiislamu.
Amesema kuwa Waislamu wanawajibika kuweka wazi sifa za harakati ya Imam Hussein na kueleza mapambano yake. Vilevile ametoa wito wa kufanyika mkutano wa kimataifa utakaofafanua zaidi tukio la Ashura na harakati ya Imam Hussein katika ardhi ya Karbala ambao utahudhuriwa na wasomi na wanafikra wa nchi mbalimbali duniani. 711965