IQNA

Wizara ya Wakfu ya Palestina yalaani hujuma ya Wazayuni dhidi ya Msikiti wa Yunus (as)

20:50 - March 05, 2011
Habari ID: 2090581
Wizara ya Wakfu na Masuala ya Dini ya Palestina imelaani hujuma iliyofanywa na walowezi wa Kizayuni dhidi ya Msikiti wa Nabii Yunus (as) katika kitongoji cha Halhul huko kaskazini mwa mji wa al Khalil katika Ukingo wa Magharibi mwa mto Jordan.
Wizara ya Wakfu ya Palestina imetoa taarifa ikilaani hujuma hiyo ya walowezi wa Kizayuni dhidi ya maeneo matakatifu ya Kiislamu na kutangaza kwamba jInai hiyo imetekelezwa kwa idhini ya utawala haramu wa Israel.
Imesema walowezi wa Kiyahudi waliambatana na askari usalama wa Israel ili kukabiliana na upinzani wa aina yoyote wa Waislamu wa Kipalestina kwa ajili ya kutetea Msikiti wa Nabii Yunus (as).
Taarifa hiyo imeongeza kuwa uhalifu wa maghasibu hao haukuishia hapo kwani walowezi hao waliokuwa wakipewa himaya ya askari usalama wa Israel walibeba silaha kwa ajili ya kuwatia hofu na woga wananchi wa Palestina.
Taarifa hiyo ya Wizara ya Wakfu ya Palestina imemalizia kwa kusema kuwa hujuma hiyo ya walowezi wa Kizayuni imezijeruhi hisia za Waislamu na imewataka viongozi wa nchi za Kiislamu kulinda matukufu ya dini hiyo huko Palestina mbele ya dharau na hujuma za maadui Wazayuni. 757486
captcha