Kwa mujibu wa mwandisho wa IQNA, Jumuiya ya Haki za Binadamu Nigeria
mbali na kulaani pendekezo hilo la Rais Buhari imesema sera kama hiyo ni
njia ya kukwepa utatuzi wa matatizo ya kimsingi ya nchi hiyo. Nayo
Jumuiya ya Mawakili Nigeria (NBA) imesema kupigwa marufuku vazi la
kujisitiri wanawake Waislamu yaani Hijani ni kinyume cha katiba ya nchi
hiyo. Okey Wali mkuu wa Jumuiya hiyo amesema serikali inapaswa kutafuta
suluhisho la kudumu na la amani kuhusu changamoto za usalama nchini humo
.
Kauli hizo zimetolewa baada ya serikali kusema kuwa baadhi ya wanaotekeleza hujuma za kigaidi ni wanawake wanaovaa Hijabu.
Wali amesema kupiga marufuku Hijabu kwa msingi huo si hatua chanya wala
suluhisho la kudumu la ukosefu wa usalama. Amesema kwa mujibu wa katiba
ya Nigeria, kila mtu ana haki ya kuvaa mavazi kwa mujibu wa dini yake
na hivyo hakuna uwezekano wa kuwazuia wanawake Waislamu kuvaa Hijabu.
Hiyo juzi baada ya kupuuza mauaji yaliyofanywa na jeshi la Nigeria
dhidi ya Waislamu katika mji wa Zaria, Rais Muhammadu Buhari ametoa
matamshi yaliyowashangaza wengi na kusema iwapo italazimu atapiga
marufuku vazi la mwanamke wa Kiislamu la hijabu.
Rais Buhari aliongeza kuwa, serikali yake haina njia nyingine ghairi ya
kuchagua moja kati ya mambo mawili ama vazi la hijabu au usalama na
kwamba yeye atalipiga marufuku vazi hilo la staha la mwanamke wa
Kiislamu nchini Nigeria.
Buhari amesema wanawake hawapasi kuvaa hijabu kwa sababu vazi hilo linatumiwa kulipua mabomu na kwamba wanawake hao ni magaidi.
Baada ya mauaji yaliyofanywa na jeshi la Nigeria wiki kadhaa zilizopita
katika mji wa Zaria wanawake wengine wametiwa nguvuni na kuvuliwa vazi
lao la hijabu katika korokoro za nchi hiyo. Hii ni licha ya kwamba
inakadiriwa kuwa asilimia kubwa ya Wanigeria ni Waislamu. Hatua za hivi
karibuni za serikali ya Nigeria zimefichua mkono wa Wazayuni na Marekani
dhidi ya Waislamu nchini Nigeria.
Tarehe 13 Disemba jeshi la Nigeria lilishambulia vituo vya Harakati ya
Kiislamu Nigeria Sheikh Ibrahim Zakzaky na kuua mamia ya Waislamu na
kisha kumtia mbaroni kiongozi huyo.