Ayman Abdul-Qadir, ameyasema hayo Alkhamisi na kuongeza kuwa, hadi sasa ndege hizo za Saudia zimekwishafanya mashambulizi dhidi ya misikiti 136 mjini Sana'a pekee. Ameongeza kuwa, ripoti za awali zinaonyesha kuwa, katika hujuma hizo jumla ya misikiti 49, imebomolewa kikamilifu na misikiti mingine kadhaa imeharibiwa vibaya. Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Idara ya Utamaduni na Wakfu mjini Sana'a, zaidi ya asilimia 80 ya misikiti imebomolewa. Aidha amesema kuwa, mbali na misikiti, ndege hizo za Aal Saud zimeyalenga maeneo yenye historia na tamaduni za kidini za Yemen likiwemo jengo la historia ya ujenzi wa misikiti na ziara la 'al-Imam Aswan'aani' lililoko mjini Sana'a lenye umri wa mamia ya miaka.
Ayman Abdul-Qadir amelaani vikali mashambulizi hayo ya kichokozi ya Saudi Arabia dhidi ya maeneo ya kidini na makazi ya raia na amezitaka taasisi za haki za binaadamu za kimataifa kuulazimisha utawala wa kifalme wa Saudia ukomeshe mashambulizi hayo ambayo yanakinzana na misingi ya kidini na kibinaadamu. Itakumbukwa kuwa, hujuma za Aal Saud nchini Yemen, zilianza tarehe 26 mwezi Machi mwaka jana, kwa lengo la kuwalazimisha Wayemen wamkubali rais mtoro na aliyejiuzulu uongozi, Abd Rabbuh Mansur Hadi, njama ambazo zimeishia kufeli licha ya kutekeleza jinai na mauaji ya kutisha nchini humo. Tangu wakati huo hadi sasa, zaidi ya watu 8,500 wameuawa na wengine karibu elfu 16 wamejeruhiwa. Aghalabu ya waliouawa au kujeruhiwa katika vita vya Saudia nchini Yemen ni wanawake na watoto.