Ayatullah Sayyid Ali Khamenei amesema hayo leo Alkhamisi katika ujumbe aliotuma kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter kwa lugha za Kiurdu, Kiingereza na Kifarsi ambapo amelaani vikali mauaji ya makumi ya Waislamu katika ghasia zinazoendelea kushuhudiwa katika mji mkuu wa India, New Delhi tokea Februari 23.
Katika ujumbe huo, Ayatullah Khemenei amesema, "nyoyo za Waislamu wote kote duniani zinaomboleza na kusikitika kutokana na mauaji ya halaiki ya Waislamu nchini India."
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameitaka serikali ya India ipambane na Wahindu wenye misimamo mikali na vyama vyao, na kukomesha mauaji ya Waislamu ili kuzuia India isitengwe katika ulimwengu wa Kiislamu. Ayatullah Sayyid Ali Khamenei amemalizia ujumbe huo kwa kutumia alama ya reli (hashtegi) na kuandika #WaislamuWaIndiaKatikaHatari.
Sheria mpya ya uraia nchini India inaruhusu kupewa uraia wahajiri wasio Waislamu waliokimbilia nchini humo kutoka nchi jirani za Bangladesh, Pakistan na Afghanistan, huku ikiwanyima haki hiyo ya uraia Waislamu.
Sheria hiyo imepingwa na jamii ya Waislamu nchini humo, asasi za kiraia na hata baadhi ya wanachama waandamizi wa chama tawala nchini humo cha Bharatiya Janata (JBP) ambao wanasema kuwa, sheria hiyo ni ya kibaguzi.