IQNA

Hofu ya makombora ya harakati ya Ansarullah yapelekea Netanyahu afute safari yake UAE

20:57 - March 15, 2021
Habari ID: 3473736
TEHRAN (IQNA)- Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni amesema kuwa amefuta safari yake katika Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati) kwa kuhofu mashambulizi ya makombora ya Harakati ya Ansarullah ya Yemen.

Akizungumza na kanali ya 13 ya televisheni ya utawala wa Kizayuni, Benjamin Netanyahu amesema kuwa, wiki iliyopita Jordan ilifunga anga yake kwa muda na kuizuia ndege ya Netanyahu kuruka; na kwa sababu hiyo  kulikuwa na njia nyingine moja tu ya kusafiri kwenda Imarati  ambayo ilikuwa ni  kutumia njia ya anga ya Saudi Arabia. 

Katika mahojiano hayo Netanyahu ameashiria mashambulizi ya makombora ya Wayemeni dhidi wanajeshi wa muungano vamizi unaoongozwa na Saudia na kuongeza kuwa, wiki iliyopita matatizo yalijitokeza katika anga ya Saudi Arabia. 

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu hata hivyo hakutoa maelezo zaidi kuhusu kukumbwa na matatizo anga ya Saudia na wala hakusema ndege yake ilitishiwa kulengwa na mashambulizi ya Ansarullah au la. Netanyahu alitazamia kukutana na Mohammed bin Zayed Al Nahyan mrithi wa mtawala wa Abu Dhabi katika safari yake  ambayo aliipanga kuifanya huko Imarati wiki iliyopita. 

Wapiganaji wa Harakati ya Ansarullah na jeshi la Yemen hivi karibuni walijibu hujuma na mashambulizi mtawalia ya Saudi Arabia kwa kuishambulia moja ya bandari za mafuta za nchi hiyo kwa kutumia makombora na ndege zisizo na rubani; mashambulizi hayo yalisababisha kusitishwa safari za ndege katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jeddah. 

Awali ilielezwa kuwa sababu iliyopelekea kufutwa safari ya Netanyahu huko Imarati ni kitendo cha viongozi wa utawala wa Kizayuni cha kumzuia mrithi wa kiti cha ufalme wa Jordan kuingia katika msikiti wa al Aqsa; jambo lililowakasirishwa viongozi wa Jordan.   

3959677

captcha