Televisheni mbalimbali za kieneo na kimataifa zimeonesha idadi kubwa ya miili ya watu ikiwa imeenea kwenye mitaa ya eneo hilo huku maafisa wa magari ya wagonjwa wakikiri kuwa wamezidiwa na idadi ya watu wanaosubiri huduma zao. Walioshuhudia wanasema kuwa, hakuna hata mwanajeshi mmoja wa Kipalestina aliyekuwemo katika watu waliouliwa kinyama na Wazayuni huko Shujaiya.
Wanamapambano wa Palestina kupitia vyombo vyao vya habari kama vile televisheni ya al Aqsa wamesema kuwa watalipiza kisasi cha jinai hizo mpya kabisa za utawala wa Kizayuni wa Israel. Tayari wanamapambano wa Palestina wameushambulia kwa makombora mji wa Beyt Yam wa karibu na mji mkuu wa utawala wa Kizayuni, Tel Aviv pamoja na mji wa Be'er Sab'i kwa makombora aina ya M75 na Sijjil 55 ikiwa ni kutekeleza ahadi zao kwa wananchi wa Palestina kuwa hawatoacha jinai za Wazayuni zipite vivi hivi.
Hadi sasa Wapalestina zaidi ya 500 wameuawa shahidi tokea Julai 8 wakati utawala wa Kizayuni wa Israelulipoanzisha hujuma ya kinyama dhidi ya Wapalestina katika eneo la Ukanda wa Ghaza. Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa zaidi ya silimia 80 ya waliouawa katika hujuma hizi ni raia wakiwemo wanawake na watoto wachanga.