Kikao cha kimataifa cha 'wanachuo wa Kiislamu na uungaji mkono kwa Gaza' kimeanza nchini Kuwait kwa udhamini wa Umoja wa Kiislamu wa Jumuiya za Wanachuo. Gazeti la Kuwait la al-Qabas limeripoti kwamba, wawakilishi na viongozi wa jumuiya mbalimbali za Kiislamu wameshiriki kwa wingi katika kikao hicho.
Abubakr Abdul Fatah, Katibu Mkuu wa umoja huo wa jumuiya za Kiislamu amesema kuwa lengo kuu la kufanyika kikao hicho ni kuchunguza njia za kukarabatiwa haraka shule na vyuo vikuu vya Gaza vilivyoharibiwa hivi karibu na utawala haramu wa Israel katika mashambulio yake ya kinyama dhidi ya watu wasio na hatia wa ukanda huo, na kuendelea kutolewa misaada ya kibinadamu kwa watu walioathiriwa na vita hivyo.
Abubakr Abdul Fatah ameongeza kuwa, ushirikiano na jumuiya pamoja na taasisi mbalimbali za kimataifa kwa madhumuni ya kufikisha misaada ya kibinadamu kwa wahitaji na kuratibiwa misimamo ya jumuiya zote za wanachuo kuhusiana na suala la Gaza ni miongoni mwa malengo mengine ya kikao hicho cha Kuwait.
Amesema, jumuiya hizo zimekuwa zikifanya maandamano makubwa tokea kuanza kwa mashambulio ya kinyama ya Wazayuni dhidi ya wakazi wasio na ulinzi wa Gaza na kuratibu njia za kupunguza machungu ya watu walioathirika kutokana na mashambulio hayo ya kinyama. Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limetangaza kuwa wanafunzi wa Palestina wanahudhuria masomo siku chache sana shuleni kutokana na masuala ya kiusalama, kuwekewa vikwazo na mzingiro, kufyatuliwa risasi na kudondoshewa mabomu mara kwa mara na askari wa utawala haramu wa Israel. 350774