Akizungumza katika swala ya Ijumaa ya wiki hii huko Lebanon, Muhammad Rashid Qabbani, Mufti wa Lebanon amelaani shambulio la kigaidi la hivi karibuni huko Alexandria nchini Misri na kusema kuwa mafundisho ya Kiislamu na Qur'ani yanawataka Waislamu kuishi pamoja kwa amani na wenzao wa Kikristo.
Akizungumza katika Msikiti wa Muhammad Amin huko Beirut, mji mkuu wa Lebanon, Sheikh Qabbani amesema kuwa kushambuliwa Wakristo na kujihusisha na vitendo vya kigaidi ni jambo linalokwenda kinyume kabisa na mafundisho ya dini tukufu ya Kiislamu.
Huku akisisitiza kwamba mikono ya maadui wa kigeni inaonekana wazi katika tukio hilo la kusikitisha, Sheikh Qabbani amesema kuwa Qur'ani Tukufu daima inawasihi Waislamu kufanya mazungumzo na kuishi pamoja kwa amani na wafuasi wa dini nyinginezo za mbinguni na kwamba kuhusishwa vitendo vya kigaidi na Waislamu ni njama inayofanywa na maadui kwa ajili ya kuchafua jina la Uislamu.
Fuad Siniora, Waziri Mkuu wa zamani wa Lebanon, Muhammad Raheemov, mwakilishi wa Mufti wa Russia nchini Lebanon, wabunge na viongozi wa kidini pamoja na maafisa wa serikali walihudhuria swala hiyo. 726323