IQNA

Harakati ya Nahdhatul Islamiya yatambuliwa rasmi Tunisia

16:05 - March 02, 2011
Habari ID: 2089347
Ali al-Aridh Msemaji wa serikali ya mpito ya Tunisia alitangaza jana Jumanne kuwa harakati ya Kiislamu ya Nahdhatul Islamiya sasa inatambuliwa rasmi na serikali hiyo baada ya kupita miaka 30 ya kuasisiwa kwake na kwamba inaweza kuanzisha chama rasmi cha kisiasa nchini.
Harakati hiyo imetambuliwa rasmi na kupewa kibali cha kuendesha shughuli zake na Wizara ya Mambo ya Ndani mara tu baada ya kujiuzulu Muhammad Ghanushi, Waziri Mkuu wa serikali ya mpito ya Tunisia na kuchukuliwa nafasi yake na al-Baji Faid as-Sibsi.
Harakati ya an-Nahdha iliasisiwa nchini Tunisia mwaka 1981 na Rashid Ghanushi pamoja na wasomi kadhaa wa Tunisia waliokuwa wameathirika na harakati ya Ikhwanul Muslimeen nchini Misri.
Harakati hiyo ilipigwa marufuku mwaka 1989 na serikali dhalimu ya dikteta Zeinul Abedeen bin Ali aliyeng'olewa madarakani hivi karibuni na wimbi la maandamano ya wananchi, baada ya kushiriki kwenye uchaguzi wa bunge na kujishindia asilimia 17 ya kura zilizopigwa. Baada ya hapo wanachama wake wengi walikandamizwa, kuteswa na kufungwa jela.
Rashid Ghanushi aliruhusiwa kurejea nchini Tunisia hivi karibuni baada ya kulazimika kuishi uhamishoni kwa kipindi cha miaka 20. 756479
captcha