IQNA

Mamdani kutafakari kumkamata Netanyahu wakati wa mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa

17:18 - July 19, 2026
Habari ID: 3482506
IQNA – Meya wa Jiji la New York, Zohran Mamdani, amesema Jumamosi kuwa utawala wake unachunguza iwapo una mamlaka ya kisheria ya kumkamata Waziri Mkuu wa utawala haramu wa Israel, Benjamin Netanyahu, iwapo atatembelea jiji hilo kwa ajili ya Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa mwezi Septemba.

“Ninaamini kuwa Waziri Mkuu Netanyahu anastahili kuwepo The Hague,” Mamdani alisema katika podikasti ya ‘The Interview’ ya gazeti la The New York Times. “Yeye ni mhalifu wa kivita ambaye anasakwa na Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC).”

Mamdani ameeleza kuwa yupo katika “mazungumzo ya kina” na Idara ya Sheria ya Jiji la New York ili kubaini kama anayo mamlaka ya kutoa amri kwa Polisi wa New York (NYPD) kumtia kizuizini kiongozi huyo wa kigeni.

“Chochote ambacho sheria inaniruhusu kufanya katika Jiji la New York, ndicho tutakachokifanya, lakini hatutajitungia sheria zetu wenyewe kwa ajili ya kufanikisha hilo,” alisema.

Katika kampeni zake za kugombea umeya, Mamdani alikuwa amesema awali kuwa atatafuta njia ya kutekeleza hati ya kukamatwa kwa Netanyahu iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) iwapo Netanyahu angezuru New York.

Mamdani amekuwa akilaani mara kwa mara vita vya kimbari vinavyofanywa na utawala wa Israel dhidi ya watu wa Gaza.

3498327

Habari zinazohusiana
captcha