IQNA

Spika wa Bunge la Iran akosoa sera za kindumakuwili za Magharibi

12:02 - June 19, 2011
Habari ID: 2140216
Spika wa Bunge la Iran amekosoa sera za kiundumakuwili za Wamagharibi kuhusu harakati za kidemokrasia katika eneo la Mashariki ya Kati na kuongeza kuwa utawala katili wa Israel unaendeleza unyama wake chini ya himaya kamili ya Marekani na baadhi ya nchi za Magharibi.
Ali Larijani Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameongeza kuwa nchi za bara Asia zinakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo zinalifanya lisiendelee, ikiwemo changamoto inayohusiana na masuala ya kielimu. Akizungumza Jumamosi ya jana katika Bodi ya Utendaji katika Kongamano la Mabunge ya Asia kwa ajili ya Elimu, Larijani ameeleza kuwa karibu nusu ya watu wazima duniani ambao hawana elimu wanaishi katika bara Asia. Spika Larijani pia amesema kwamba bara Asia linakabiliwa na matatizo mbalimbali kama vile athari mbaya za mgogoro wa uchumi, umasikini, ustawi duni wa uchumi, utapiamlo, ukosefu wa usalama wa chakula, matatizo ya kiutamaduni, majanga ya kibinadamu na kubwa kuliko yote ni kukaliwa kijeshi baadhi ya maeneo ya bara hili.
Spika wa Bunge la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran aidha amesema, iwapo nchi kama Afghanistan, Iraq, Bahrain na ardhi zinaokaliwa kwa mabavu za Palestina zitaendelea kudhibitiwa na wageni hakutakuwepo uwezekano wa kupatikana maendeleo kwenye maeneo hayo.

810660
captcha