Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Hizbullah ya Lebanon imelaani mashambulio ya kijeshi ya utawala haramu wa Israel katika Ukanda wa Gaza na kusisitiza kwamba, mashambulio hayo ni mwendelezo wa jinai za utawala huo ghasibu dhidi ya wananchi wa Palestina.
Taarifa ya Hizbullah imebainisha kwamba, kuendelea kimya cha nchi za Kiarabu na uzembe wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu katika kukomesha jinai za Israel huko Palestina kumezifanya jinai za Tel Aviv kuchukua mkondo mpya.
Hizbullah ya Lebanon imeashiria pia hatua isiyo ya kiutu ya asasi za kimataifa hususan Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ya kutoonyesha radiamali yoyote kwa jinai za Israel na kusisitiza kwamba, asasi hizo sio tu kwamba, hazizuii jinai za Israel bali zipo pamoja nayo na zinawasaidia Wazayuni maghasibu katika kuwauwa wananchi wasio na ulinzi wa Palestina.
Wapalestina watano wameuawa shahidi na makumi ya wengine kujeruhiwa kufuatia mashambulio ya anga ya siku mbili ya Israel katika maeneo tofauti ya Ukanda wa Gaza, huko Palestina. 912480