Kwa mujibu wa mwandishi wa IQNA, wanajeshi na masetla hao waliuhujumu Msikiti wa Al Aqsa kupitia mlango wa Bab al Maghareba na kuivunjia heshima sehemu hiyo ya ibada.
Wazayuni hao aidha waliwatisha watoto wa Kipalestina waliokuwa hapo.
Tangu ulipoasisiwa, utawala haramu wa Kizayuni wa Israel umeshabomoa kikamilifu mamia ya misikiti na kuharibu mamia ya mingine. Mwaka 1969, katika njama iliyotekelezwa kwa uratibu wa viongozi wa utawala haramu wa Israel, Wazayuni wenye misimamo ya kufurutu ada wakiongozwa na Denis Michael Rohan waliuchoma moto msikiti wa al Aqsa na kuziharibu vibaya baadhi ya sehemu za msikiti huo. Katika kufanikisha njama yake hiyo ya kukifuta kibla hicho cha kwanza cha Waislamu, utawala wa Kizayuni umeshachukua pia hatua za kuchimba njia kadhaa za chini kwa chini kandokando na chini ya ua wa mahali hapo patakatifu.
Masuala haya yanaonesha kuwa hatua za hujuma na uharibifu za utawala wa Kizayuni dhidi ya msikiti wa al Aqsa zimechukua sura hatari zaidi. Pamoja na hayo wananchi wa Palestina wameonesha kuwa hawako tayari kuvumilia njama za utawala haramu wa Israel dhidi ya matukufu ya Kiislamu. Intifadha ya Quds ya mwaka 2000 iliyoanza baada ya kitendo cha kishenzi cha Sharon cha kujusuru kuingia ndani ya uwanja wa msikiti wa al Aqsa ni ithbati tosha juu ya suala hilo
1049178