IQNA

Rais Ahmadinejad: Mwanamke ana mchango mkubwa katika jamii

11:14 - July 11, 2012
Habari ID: 2365980
Rais Mahmoud Ahmadinejad wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema katika sherehe za ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa Wanawake na Mwamko wa Kiislamu ulioanza leo hapa Tehran kuwa wanaume na wanawake wanashirikiana katika asili ya kuumbwa lakini mwanamke amekuwa na mchango mkubwa zaidi na wenye taathira kubwa zaidi ya ule wa mwanaume katika matukio ya kijamii.
Amesema kuwa matunda yote ya mwanadamu yametokana na juhudi za mama na kuongeza kuwa kila mwanaume aliyefikia kilele cha mafanikio amefikia nafasi hiyo kutokana na juhudi za mama aliyemlea au mwanamke aliyemsaidia. Ameongeza kuwa ni muhali katika jamii yoyote mwanamke atake mabadiliko na yasifanyike.
Rais Ahmadinejad amesema kuwa nchi za kibeberu duniani zinapiga nara za uongo na kupora matunda na maliasili za mataifa mengine.
Rais Mahmoud Ahmadinejad amesema kuwa mabeberu wa dunia wanapiga nara za eti kulinda haki za binadamu, uhuru na kuyalinda mataifa ya ulimwengu, kutoa ahadi za kuwaletea walimwengu maisha bora na maendeleo katika nchi zao, ustawi wa kisiasa na kiuchumi lakini lengo lao kuu ni kupora maliasili na utajiri wa nchi hizo. Rais Ahmadinejad amesisitiza kuwa dunia ya leo inahitaji mabadiliko ya kimsingi na kuongeza kuwa sharti kuu la mabadiliko hayo ni mwamko wa Kiislamu.
Mkutano wa Kimataifa wa Wanawake na Mwamko wa Kiislamu unahudhuriwa na zaidi ya wanawake 1300 wanaojumuisha wanaharakati wa masuala ya kisiasa na kijamii kutoka nchi 85 duniani.

1049487

captcha