Akihutubia halaiki kubwa ya wananchi hapa Tehran leo Jumatano, Kiongozi Muadhamu amesema kuwa, 'vikwazo vimeiletea nchi hii matatizo lakini adui akiweka masharti ya kuondolewa vikwazo ikiwa ni pamoja na Iran kulegeza msimamo kuhusu masuala ya kimsingi kama Uislamu, uhuru au ustawi wa Kisayani, hakuna afisa yeyote mwenye fahari ya kitaifa atakayekubali kufanya hivyo.'
Kiongozi Muadhamu amesema njia pekee ya Iran kukabiliana na nguvu za adui ni nchi hii kujikinga na vikwazo. Ayatullah Khamenei amesisitiza umuhimu wa kuhakikisha uchumi wa Iran hautegemei pato la mafuta ya petroli. Ameongeza kuwa maafisa wa nchi wanapaswa kufahamu kuwa adui ataendeleza uhasama wake iwapo Iran italegeza msimamo hata chembe. Ameongeza kuwa, Iran inapaswa kuchukua hatua ambazo nchi hii itastawi, kuendelea na wananchi kupata maisha mazuri hata kama adui haondoi vikwazo. Kiongozi Muadhamu amewalaani watawala wa Marekani kutokana na kile alichokitaja kuwa ni kelele zao zisizo na aibu kwamba hawataondoa vikwazo dhidi ya Iran kwa pamoja hata kama Tehran itaafiki baadhi ya masuala kuhusu miradi yake ya nyuklia. Kiongozi Muadhamu ameongeza kuwa hapingi suala la kuendelea mazungumzo ya nyuklia baina ya Iran na madola sita makubwa duniani lakini ameongeza kwamba, anaamini kunapaswa kufikiwa nukta yenye kuleta matumaini katika mazungumzo hayo.../mh