IQNA

Iran yataka dunia iunge mkono wananchi wanaodhulumiwa wa Palestina

15:05 - May 15, 2020
Habari ID: 3472767
TEHRAN (IQNA) - Wizara ya Mambo ya Nje Iran imetoa tamko kuhusu siku ya "Nakba" yaani siku ya nakama ya kuasisiwa utawala pandikizi wa Kizayuni katika ardhi walizoporwa Wapalestina na kusisitiza kuwa, kadhia ya Palestina itaendelea kuwa suala kuu nambari moja katika ulimwengu wa Kiislamu licha ya kufanyika njama nyingi za kulisahaulisha.

Jana tarehe 14 Mei inasadifiana na mwaka wa 71 wa kufukuzwa mamia ya maelfu ya Wapalestina kwenye ardhi zao na kesho yaani tarehe 15 Mei, utawala pandikizi wa Kizayuni uliopachikwa jina bandia la Israel, utatimiza miaka 71 tangu kupandikizwa kwake kwenye ardhi hizo za Wapalestina. Katika tamko lake hilo, Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran imeitaka Jumuiya ya Ushirikiano wa Kiislamu OIC, tawala na wananchi wa nchi za Kiislamu na mataifa mengine huru duniani kuchukua hatua za maana za kuwaunga mkono wananchi wanaodhulumiwa wa Palestina na kuwasaidia kukomboa ardhi zao zinazokaliwa kwa mabavu na Wazayuni.

Tamko hilo limeashiria pia jinai zinazofanywa na utawala wa Kizayuni kwa zaidi ya miaka 70 sasa na kuongeza kuwa, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran itaendelea kuunga mkono kikamilifu malengo matukufu ya wananchi wa Palestina, kuwaenzi mashahidi na wanajihadi wa taifa hilo ambako ndiko kiliko Kibla cha Kwanza cha Waislamu na vile vile itaendelea kupinga mipango yote ya kujidhalilisha kwa Wazayuni, kama ambavyo inapinga vikali pia mpango wa kidhulma wa "Muamala wa Karne" uliopendekezwa na dola la kibeberu la Marekani kwa nia ya kuiangamiza kikamilifu kadhia ya Palestina. 

Vile vile katika tamko lake hilo, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imezitaka taasisi na mashirika ya kimataifa hususan Umoja wa Mataifa kutekeleza majukumu yao ya kukomeshwa kukaliwa kwa mabavu ardhi za Palestina na kuandaa mazingira ya kuweza wakimbizi wa Kipalestina kurejea katika ardhi za mababu zao.

3898846

captcha