IQNA

Siasa

Bunge la Iran laidhinisha mawaziri wote waliopendekezwa na Rais Pezeshkian

23:57 - August 21, 2024
Habari ID: 3479311
IQNA-Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu (Bunge la Iran) imehitimisha mjadala kuhusu baraza jipya la mawaziri la serikali ya awamu ya 14 kwa kuidhinisha mawaziri 19 waliopendekezwa na Rais Masoud Pezeshkian.

Wabunge Jumatano walipiga kura ya kuunga mkono mawaziri wote waliopendekezwa na rais baada ya siku tano za vikao na majadiliano.

Mnamo Agosti 11, siku 12 baada ya hafla ya kuapishwa kwake rais Pezeshkian aliwasilisha orodha ya mawaziri bungeni ili kuchunguzwa na kupigiwa kura ya imani

Ikumbukwe kuwa kufuatia ajali mbaya ya helikopta iliyosababisha kifo cha Rais Ebrahim Raisi mnamo Mei 19, Pezeshkian aliibuka kuwa mmoja wa wagombea sita wa mwisho waliochaguliwa na Baraza la Kulinda Katiba kutoka miongoni mwa kundi la watu 80 waliokuwa wamejiandikisha kugombea urais.

Alipata kura nyingi zaidi katika duru ya kwanza ya uchaguzi wa rais mnamo Juni 28 ambapo hakuna mshindi mutlaki aliyepatikana na hivyo na akapambana na mshindi wa pili, Saeed Jalili, katika marudio ya uchaguzi wa Julai 5Pezeshkian ambaye ni daktari wa moyo alishinda duru ya pili kwa kupata 53.66% ya kura.

Akizungumza Jumapili wakati alipofika bungeni kuteta baraza lake la mawaziri, Rais Pezeshkian alisema: “Baraza la mawaziri lililowasilishwa bungeni leo ni serikali ya umoja wa kitaifa; serikali ya umoja wa kitaifa ni serikali inayojiona kuwa serikali ya watu wote wa Iran. Serikali ya umoja wa kitaifa ina wajibu wa kutetea haki za raia za Wairani wote na imejitolea kuweka kipaumbele kwa maslahi ya kitaifa kuliko maslahi mengine yoyote."

4232565

captcha