Mohammad Jawad Zarif ameyasema hayo leo Jumanne mjini Tehran wakati alipohutubia kikao cha saba cha Baraza Kuu la Jumuiya ya Radio na Televisheni za Kiislamu. Ameongeza kuwa, dunia imeshaondoka katika mfumo wa kidhalimu wa kambi mbili na sasa inaelekea katika mfumo mpya. Amesema katika mfumo huu mpya wa kimataifa mbali na serikali pia sasa kuna washirika wengine kama vile vyombo vya habari ambavyo vitakuwa na nafasi muhimu katika kipindi hiki cha mpito. Zarif amesema Jumuiya ya Radio na Televisheni za Kiislamu ina nafasi muhimu katika ulimwengu wa Kiislamu. Ameongeza kuwa jumuiya hiyo inapaswa kutafuta njia za kuhimiza misimamo ya wastani na matumaini ya kuwepo amani katika umma wa Kiislamu kwa msingi wa izza na haki hasa haki za kuainisha hatima ya mataifa na hususan taifa linalodhulumiwa la Palestina. Zarif amesisitiza kuwa Jumuiya ya Radio na Televisheni za Kiislamu ni fursa ya kuleta sauti moja katika umma wa Kiislamu kote duniani. Aidha ametoa wito kwa vyombo vya habari vya Kiislamu kuwaelimisha walimwengu kuwa kile ambacho kinatajwa kuwa misimamo mikali ya kidini haifungamani na Uislamu.