Aziz Kadhim Alawan, mkuu wa zamani wa mkoa wa Dhiqar nchini Iraq amezungumzia habari ya kuanzishwa hivi karibuni Kituo cha Kimataifa cha Mazungumzo kati ya Dini mbalimbali huko katika mji wa Nasiriyya, ambayo ni makao makuu ya mkoa huo wa kusini magharibi mwa Iraq.
Kwa mujibu wa gazeti la Iraq la As-Swabah, Alawan amesema kuwa, kuna mijengo na athari nyingi za kidini na kihistoria za makanisa mbalimbali katika mji huo, jambo linalofanya uamuzi wa kijenga kituo hicho cha kimataifa cha mazungumzo ya kidini kuwa na umuhimu mkubwa. Amesema kuwa mji huo una majengo muhimu ya kidini ikiwemo nyumba ya kale ya Nabii Ibrahim (as) jambo ambalo amesema kuwa litawavutia sana wafuasi wa dini tofauti za mbinguni.
Aziz Kadhim Alawan ameongeza kuwa, mji huo una vivutio vingine vya kitalii na kimaumbile ambavyo amesema ana uhakika vitawavutia watu wengi duniani.
Ismail al-Abudi, mkuu wa jumuiya ya uwekezaji ya mkoa uliotajwa pia amesema kuhusiana na suala hilo kwamba, kuna miradi 52 muhimu inayotekelezwa katika mji huo kwa lengo la kukarabati athari za kidini, kihistoria na kitalii ili kuvutia watalii katika mkoa huo. 399374