Maonyesho ya 18 ya Kimataifa ya Qur'ani Tukufu ya Tehran, Iran yamefunguliwa rasmi Jumamosi katika ukumbi wa sala wa Imam Khomeini katika sherehe zilizohudhuriwa na mwanazuoni wa ngazi za juu Hujjatul Islam Sayyid Ahmad Alamulhuda na Waziri wa Utamaduni na Miongozo ya Kiislamu Dkt. Sayyed Muhammad Husseini.
Sherehe hizo zimeanza kwa kiraa ya Qur'ani Tukufu iliyosomwa na Saeed Tusi, qari wa kimataifa wa Iran.
Akizungmza katika sherehe hizo, Mkuu wa Kitengo cha Masuala ya Qur'ani katika Wizara ya Utamaduni na Miongozo ya Kiislamu, Hujjatul Islam Hamid Mohammadi ambaye pia ni mkuu wa maonyesho ya mwaka huu amesema, ‘kwa mara ya kwanza katika historia ya Uislamu, kunashuhudiwa himaya kubwa katika shughuli za Quran Tukufu na bajeti kubwa imetengwa kwa ajili ya sekta hiyo'. Amesema Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu, yaani bunge la Iran, imepitisha muswada wa kutenga bajeti kwa ajili ya shughuli za Quran Tukufu. Maonyesho ya 18 Kimataifa ya Qur'ani Tukufu yana washiriki kutoka nchi 25 duniani. Kaulimbiu ya maonyesho ya mwaka huu ni "Qur'ani, Kitabu cha Maisha". Maonyesho hayo yataendelea hadi tarehe 23 ya mwezi mtukufu wa Ramadhani.
628407