Kwa mujibu wa tovuti ya alqubanchi, Sayyid Qubanchi ambaye alikuwa akizungumza katika hotuba za swala ya Ijumaa huko katika Husseiniyya ya al-Fatimah katika mji mtakatifu wa Najaf amekosoa kejeli inayofanywa na baadhi ya viongozi wa Iraq kuhusiana na makundi ya kumuomboleza Imam Hussein (as) kwa kuyataja kuwa yasiyostaarabika.
Amesema Imam Hussein (as) ni nembo halisi ya ustaarabu wa Kiislamu na kwamba mtukufu huyo alikuwa katika mstari wa mbele wa kutetea ustaarabu, maendeleao na uhuru wa mwanadamu.
Imam huyo wa swala ya Ijumaa amelalamikia vikali dharau hiyo inayofanywa na baadhi ya watu na kusema kuwa watu kama hao waovu hawana nafasi katika mji mtakatifu wa Najaf. Ameashiria katika sehemu nyingine ya hotuba yake tukio la kuuawa shahidi Imam Swadiq (as) na nafasi yake katika kuimarisha harakati ya elimu na fikra ya Kiislamu na kuongeza kuwa Maimamu wote Watoharifu (as) walikuwa na nafasi muhimu katika kukabiliana na hatari ya fikra ya kukufurishwa Waislamu na kuimarisha fikra sahihi ya Uislamu katika umma.
Tunaashiria hapa kuwa kwa kisingizio cha kuchaguliwa Najaf kuwa mji mkuu wa kiutamaduni wa ulimwengu wa Kiislamu mwaka 2010, baadhi ya viongozi wa Iraq wametoa matamshi ya kukejeli na kuyakosea heshima makundi ya maombolezo ya Imam Hussein kwa kudai kwamba ni nembo ya kutostaarabika, jambo ambalo limewakasirisha sana maulama na wanazuoni wa Kiislamu katika mji mtakatifu wa Najaf. 667036