Kikao cha viongozi wa kidini na wanaharakati wa masuala ya kijamii, kiutamaduni na kiuchumi kilifanyika hapo siku ya Jumanne huko katika mkoa wa Tartus nchini Syria kwa lengo la kuimarisha mielekeo ya kuvumiliana na kuishi pamoja kwa amani wafuasi wa dini tofauti.
Kwa mujibu wa rtv.gov.sy, njia za kuimarishwa mazingira ya kuishi pamoja kwa amani na urafiki wafuasi wa dini za mbinguni zimechunguzwa katika kikao hicho. Shakhsia na wasomi waliozungumza katika kikao hicho walimewataka wananchi wote wa Syria kuwa waangalifu na kuzingatia maslahi ya kitaifa katika kukabiliana na matukio yanayoendelea hivi sasa nchini humo ili wasije wakatumiwa vibaya na wageni pamoja na maadui wasiopenda kuiona nchi hiyo ikiimarika na kuwa na nguvu katika uwanja wa kimataifa. Kwa mujibu wa ripoti, kikao hicho kimesisitiza juu ya nafasi muhimu ya vyombo vya habari katika kuakisi habari sahihi na kuwashajiisha wananchi wazingatie umoja na mshikamano. Waliohutubu wamesema kuwa vyombo hivyo vina nafasi muhimu ya kuunganisha wananchi na viongozi wao serikalini, na kwamba watawala wanapasa kufanya kila wawezalo ili kuwahudumia wananchi na kutatua matatizo yao. 777846