IQNA

Msemaji wa Gaddafi asema dikteta huyo wa Libya yuko salama

13:58 - September 06, 2011
Habari ID: 2182191
Musa Ibrahim, msemaji wa utawala wa dikteta Mummar Gaddafi wa Libya amesema kuwa kiongozi huyo ni mzima wa afya na kwamba anaishi kwa amani katika moja ya miji ya nchi hiyo.
Huku akidai kwamba watu aliowataja kuwa ni makundi ya mifarakano hawawezi kugundua sehemu aliko dikteta huyo, Ibrahim amesema kuwa Gaddafi angali yuko nchini Libya na kwamba maadui wake hawatampata. Amesema utawala wake ungali una nguvu nchini humo na kwamba wanawe ndio wanaoendesha masuala ya nchi na kuchukua hatua zote muhimu za kuilinda nchi hiyo.
Musa Ibrahim ameongeza kuwa wanawe hao wako tayari kufa kwa ajili ya kuilinda nchi yao.
Amesema kuwa Seiful Islam mwanawe Gaddafi pia angali yuko nchini humo. Amesisitiza kwamba kamwe Libya haitaanguka mikononi mwa wanamapinduzi na kwamba makabila ya nchi hiyo yanafanya kila liwezekanalo ili kuilinda na kwamba wataendeleza mapambano yao hadi watakapokomboa miji yote iliyotekwa na wanamapinduzi. 855440
captcha