IQNA

Kufuata mafunzo ya Qur’ani ndio chanzo cha mwamko wa Kiislamu

15:52 - November 19, 2011
Habari ID: 2224106
Spika wa Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu ya Iran Dakta Ali Larijani amesema sababu ya kuendelea mwamko wa Kiislamu katika eneo la Mashariki ya Kati na kaskazini mwa Afrika ni kufuatwa mafundisho ya Qur’ani Tukufu.
Akihutubu Kongamano la Tisa la Kimataifa la Watafiti Wanawake katika uga wa Qur’ani mjini Tehran, Dr. Larijani amesema: ‘Leo tunashuhudia mwamko wa Kiislamu katika nchi kama vile Misri, Tunisia, Yemen, Bahrain n.k na jambo hili linaonyesha namna Qur’ani Tukufu ilivyo na ushawishi katika jamii’.
Larijani amesisitiza kuwa Qur’ani imeteremshwa kwa ajli ya wanadamu wote katika nyakati zote na wala hailengi zama makhsusi au watu wa kaumu au rangi maalumu.
Spika wa Bunge la Iran ameongeza kuwa wakati maadui walipojaribu kutumia propaganda kuwashawishi watu waiache Qur’ani, kinyume chake kimefanyika na watu wamerejea kwa wingi zaidi katika mafundisho ya Qur’ani Tukufu zaidi ya wakati wowote ule.
Spika Larijani pia amepongeza mafanikio ya Kongamano la Kimataifa la Wanawake Watafiti katika uga wa Qur’ani. Ameongeza kuwa moja ya baraka za Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ni kustawi harakati za utafiti wa Qur’ani miongoni mwa wanawake.
Kongamano hilo lilifanyika katika ukumbi wa Mnara wa Milad mjini Tehran Alkhamisi Novemba 17.
899871
captcha