IQNA

Rais Ahmadinejad:

Mwanamke amekuwa na mchango mkubwa katika matukio ya kijamii

17:03 - July 10, 2012
Habari ID: 2365429
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema katika sherehe za ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa Wanawake na Mwamko wa Kiislamu ulioanza leo hapa Tehran kuwa wanaume na wanawake wanashirikiana katika asili ya kuumbwa lakini mwanamke amekuwa na mchango mkubwa zaidi na wenye taathira kubwa zaidi ya ule wa mwanaume katika matukio ya kijamii.
Amesema kuwa matunda yote ya mwanadamu yametokana na juhudi za mama na kuongeza kuwa kila mwanaume aliyefikia kilele cha mafanikio amefikia nafasi hiyo kutokana na juhudi za mama aliyemlea au mwanamke aliyemsaidia. Ameongeza kuwa ni muhali katika jamii yoyote mwanamke atake mabadiliko na yasifanyike.
Rais Ahmadinejad amesema kuwa nchi za kibeberu duniani zinapiga nara za uongo na kupora matunda na maliasili za mataifa mengine.
Rais Mahmoud Ahmadinejad amesema kuwa mabeberu wa dunia wanapiga nara za eti kulinda haki za binadamu, uhuru na kuyalinda mataifa ya ulimwengu, kutoa ahadi za kuwaletea walimwengu maisha yaliyo bora na maendeleo katika nchi zao, ustawi wa kisiasa na kiuchumi ili kupora maliasili na utajiri wa nchi hizo.
Rais wa Iran amesema binadamu ameumbwa kwa ajili ya maisha aali hata hivyo lengo hilo limeshindwa kudhaminiwa. Dakta Ahmadinejad amesema kuwa baadhi ya watu wanadhani kuwa wananchi wa Marekani na Ulaya wako huru lakini ukandamizaji mbaya zaidi dhidi ya binadamu na dhidi ya raia ndio unaotawala huko Marekani.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa leo hii kundi moja la kifisadi la Wazayuni mabepari ndilo linalowatawala Wamarekani milioni 300 na mataifa mengine ya dunia nyuma ya pazia. 1049487
captcha