IQNA

Makamanda wa Iran waliowakamata wanajeshi wa Marekani wapewa nishani

19:32 - February 01, 2016
Habari ID: 3470104
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amewapa nishani makamanda wa Iran waliowakamata wanajeshi wa Marekani hivi karibuni.
Makamanda wa Jeshi la Majini la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC wamepewa nishani ya ushindi na Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Ali Khamenei ambaye pia ni Amirijeshi Mkuu wa vikosi vyote vya ulinzi vya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kutokana na makamanda hao kuwakamata wanajeshi wa Marekani walioingia katika maji ya Iran kinyume cha sheria.

Admirali Ali Fadavi, Kamanda wa Jeshi la Majini la IRGC  na makamanda wengine wanne wa jeshi hilo, waliongoza operesheni ya kishujaa ya kusimamisha na kuzikamata boti mbili za Marekani na wanajeshi kumi waliokuwemo ndani yake katika eneo la kisiwa cha Farsi cha kusini mwa Iran. Makamanda hao wa jeshi la IRGC wamepata nishani hiyo ya ushindi kutokana na operesheni yao hiyo ya kishujaa iliyofanywa haraka sana mara baada ya wanajeshi hao wa Marekani kuingia katika maji ya Iran tarehe 12 mwezi huu wa Januari kinyume cha sheria.

Aidha Amirijeshi Mkuu wa vikosi vyote vya ulinzi vya Iran amekubaliana na suala la kupandishwa cheo makamanda na maafisa wengine wa jeshi hilo walioshiriki katika operesheni hiyo kama ilivyopendekezwa na komandi kuu ya vikosi vya ulinzi nchini.

Itakukumbukwa kuwa, boti mbili za Marekani, tarehe 12 Januari 2016 zilikamatwa na wanajeshi wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC  baada ya kuingia kinyume cha sheria katika maji ya Iran na kuwatia mbaroni wanajeshi 10 wa Marekani waliokuwemo kwenye boti hizo.

Wanajeshi hao wa Marekani waliachiliwa huru baada ya kubainika kuwa waliingia kimakosa katika maji ya Iran.

3471670

captcha