IQNA

Rais Al Bashir

Sudan ilishauriwa iwe na uhusiano na Israel lakini imekataa

19:09 - January 05, 2019
Habari ID: 3471797
TEHRAN (IQNA)- Rais Omar al Bashir wa Sudan amefichua kuwa: "Tulishauriwa tuwe na uhusiano wa kawaida na Israel ili hali ya nchi yetu iboreke."

Akizungumza Alhamisi mjini Khartoum alipokutana na viongozi wa Kisufi (Twariqa), Rais wa Sudan, pasina kutoka jina la wale waliompa ushauri huo alisema: "Rizqi inatoka kwa Mwenyezi Mungu na wala haitoki kwa waja wake."

Al Bashir ameendelea kusema kuwa, kadhia ya Palestina ni ya kiitikadi na wala si ya kisiasa na kisha ameashiria maandamano ya hivi karibuni nchini Sudan na kusema: "Lengo la serikali ni kuwaletea wananchi usalama na maisha bora na tunajitahidi kufikia malengo hayo, lakini maandamano sasa yamebadilika na kuwa mgogoro."

Wakati huo huo Raisal Bashir amekanusha madai ya Waziri Mkuu wa utawala wa Kizayuni wa Israel aliyesema kuwa ndege za utawala huo zimeruhusiwa kutumia anga ya Sudan.
Rais wa Sudan amesema kuwa ,"tulipokea ombi la kutumiwa anga yetu kwa ajili ya ndege zinazoelekea Tel Aviv. Ombi hilo halikutoka kwa El Al yaani Shirika la Ndege la Israel bali lilitoka kwa Shirika la Ndege la Kenya lakini tulikataa."
Mwezi Desemba Netanyahu alidai kuwa Israel imeruhusiwa kutumia anga ya Sudan kurushia ndege zake; licha ya kwamba nchi hiyo haina uhusiano wa kidiplomasia na utawala huo ghasibu.

Tangu tarehe 19 Disemba 2018 hadi hivi sasa Sudan imekumbwa na maandamano makubwa ya nchi nzima kulalamikia hali mbaya ya kiuchumi na inasemekeana kuwa mgogoro kama huo haujawahi kuikumba Sudan katika kipindi cha zaidi ya miaka 30 iliyopita.

Omar al-Bashir amekuweko madarakani nchini Sudan tangu mwaka 1980 hadi hivi sasa. Na hii ni katika hali ambayo, wananchi wengi na vile vile makundi na vyama vya siasa nchini humo wanataka kuhitimishwa enzi za utawala wa miongo mitatu wa kiongozi huyo.

Sudan ni moja ya nchi waitifaki wa muungano vamizi wa kijeshi ulioanzishwa na Saudia katika vita dhidi ya Yemen. Omar al-Bashir alikuwa na matumaini kwamba, kwa kushiriki katika vita hivyo, atapata manufaa mengi ya kimaada kwa Saudi Arabia na Imarati; lakini alichokipata kutoka kwa tawala hizo mbili hakikuwa kikubwa kuweza kupunguza matatizo ya kiuchumi yanayoikabili Sudan.

Baada ya Omar al-Bashir kupoteza matumaini kwa waitifaki wake wapya katika Ghuba ya Uajemi, anataka kufufua uhusiano na Uturuki, Russia, Syria na Qatar; lakini muelekeo huo haujawapendeza watawala wa Israel, Saudia Arabia na Imarati.

Kwa msingi huo tunaweza kusema kuwa, kuendelea na kushamiri maandamano ya kupinga serikali nchini Sudan ni jambo linaloafikiana na maslahi ya nchi kama Saudi Arabia na Imarati ambazo ziko mbioni kuanzisha uhusiano wa kawaida na utawala haramu wa Israel.

Kwa kuzingatia sababu hayo inaelekea kuwa Sudan itaendelea kushuhudia maandamano kutokana na tawala za kigeni kutumia vibaya suala la matatizo ya kiuchumi na kisiasai kuwachochea wananchi wamiminike mitaani.

3778250

captcha