IQNA

Rais wa Zamani wa Nigeria apongeza Tafsiri ya Qur’ani kwa lugha ya Nupe

10:35 - June 28, 2026
Habari ID: 3482412
 Ibrahim Badamasi Babangida
IQNA – Rais wa zamani wa Nigeria, Ibrahim Badamasi Babangida, amepongeza kazi ya tarjuma na tafsiri ya Qur’ani Tukufu kwa lugha ya Nupe, akiieleza kuwa ni mafanikio makubwa ya kihistoria.

Babangida, aliyewakilishwa na Profesa Mohammed Kuta‑Yahaya, Makamu Mkuu wa Baraza la Chuo Kikuu cha Abdulkadir Kure mjini Minna (AKUM), aliyasema hayo siku ya Jumamosi katika mji wa Bida alipotoa hotuba yake kama Mwenyekiti wa hafla ya uzinduzi rasmi wa Qur’ani Tukufu iliyotafsiriwa kwa lugha ya Nupe.

Tafsiri hiyo imefanywa na mwanazuoni mashuhuri wa Kiislamu, Sheikh Muhammad Ibn Muhammad Pati Emisheshi, na hafla ya uzinduzi ilifanyika katika Ikulu ya Wadata.

Alisema kuwa tafsiri hiyo si tu hatua muhimu ya kidini kwa watu wa Nupe, bali pia ni mchango mkubwa katika urithi wa Kiislamu wa Nigeria kwa kufanya ujumbe wa Mwenyezi Mungu katika Qur’ani uwe rahisi zaidi kufikiwa na kueleweka na watu kupitia lugha yao ya asili.

Kwa mujibu wake, kutafsiri Qur’ani Tukufu kwa lugha za asili ni tendo la ibada lenye kujitolea kubwa pamoja na ujasiri wa kielimu, linalounganisha baina ya wahyi wa Mwenyezi Mungu na uelewa wa maisha ya kila siku.

“Tafsiri hii inawaruhusu Waumini kufahamu maana ya maneno ya Mwenyezi Mungu kwa lugha yao ya mama, jambo linaloimarisha uhusiano wao na Muumba wao na kuongeza kina cha maisha yao ya kiroho.

“Kazi hii inahakikisha kwamba ujumbe wa rehema, uadilifu, huruma na uongofu unasikika wazi katika lugha ya nyumbani, sokoni na katika jamii,” alisema.

Babangida alimpongeza Sheikh Emisheshi kwa huduma yenye thamani kubwa kwa Uislamu na kwa ubinadamu, akisema kuwa tafsiri hiyo itasaidia kuongeza uelewa wa Qur’ani kwa wale wasiobobea katika lugha ya Kiarabu.

Alibainisha kuwa mradi huo unaakisi urithi mkubwa wa Kiislamu wa watu wa Nupe na unaonyesha jinsi imani na utamaduni vinaweza kwenda sambamba katika kukuza maadili mema na maendeleo ya jamii.

Rais huyo wa zamani pia alikumbusha kuhusu historia tajiri ya elimu ya Qur’ani iliyowahi kustawi katika ardhi ya Nupe, ambapo wanazuoni walifuata mbinu ya kina ya kufundisha kwa kusoma aya za Qur’ani kwa Kiarabu, kisha kuzitafsiri kwa Kihausa na baadaye kuzifafanua kwa lugha ya Nupe.

Alisema mfumo huo uliwazalisha vizazi vya wanazuoni waliokuwa na maarifa ya kina kuhusu Qur’ani na utekelezaji wake katika maisha ya kila siku.

Kwa mujibu wake, Qur’ani hii mpya iliyotafsiriwa si mwanzo wa utamaduni mpya, bali ni kurejesha urithi mtukufu wa elimu ya Kiislamu uliokuwepo katika ardhi ya Nupe.

Babangida pia alimpongeza Etsu Nupe na Mwenyekiti wa Baraza la Watawala wa Jadi la Jimbo la Niger, Alhaji Yahaya Abubakar, kwa uongozi wake wenye maono pamoja na juhudi zake katika kuendeleza maendeleo ya kidini, kitamaduni na kielimu.

Alisisitiza kwamba zaidi ya kusoma na kukariri, Qur’ani Tukufu ni mwongozo kamili wa maisha mema, na akawahimiza Waislamu kushikamana na misingi ya uadilifu, haki, uaminifu, sadaka na huruma katika nyanja zote za maisha.

Babangida alieleza pia wasiwasi wake kwamba misukosuko na vishawishi vinavyohusiana na zama za kidijitali vimepunguza utamaduni wa kujifunza Qur’ani kwa kina, pamoja na subira na nidhamu vilivyokuwa vinawatambulisha wanazuoni wa zamani wa Kiislamu.

Hata hivyo alisema tafsiri ya Nupe inatoa fursa mpya ya kufufua utamaduni wa kujifunza Qur’ani kwa kina kwa kuwafanya watu kuelewa vyema ujumbe wa Mwenyezi Mungu.

Aliwahimiza Waislamu kuipokea tafsiri hiyo kama chombo cha kufufua upya roho za kiimani, kuamsha maadili mema na kukuza maendeleo ya jamii.

Rais huyo wa zamani pia aliwataka wasimamizi wa kazi hiyo kuhakikisha Qur’ani iliyotafsiriwa inasambazwa kwa upana, hususan katika maeneo ya vijijini ambako upatikanaji wa vitabu vya Kiislamu katika lugha za asili bado ni mdogo.

Alisema tafsiri hiyo inapaswa kuwa nyenzo madhubuti ya Da‘wah, umoja na kuishi kwa amani miongoni mwa Waislamu bila kujali tofauti za kikabila au kimadhehebu.

Aidha, aliwataka serikali katika ngazi zote, wafadhili pamoja na taasisi za Kiislamu kuunga mkono miradi kama hiyo ya kutafsiri Qur’ani Tukufu kwa lugha nyingine za Nigeria ili kukuza uelewa mpana wa Uislamu.

Mwisho, alimpongeza Sheikh Emisheshi, Baraza la Jadi la Nupe, Ikulu ya Wadata pamoja na watu wote waliochangia kukamilika kwa mradi huu wa kihistoria.

Aliomba Mwenyezi Mungu aukubali juhudi hii njema, awabariki wote waliohusika katika tafsiri hiyo, na aujaalie kuwa chanzo cha kudumu cha uongofu, amani, umoja na ustawi kwa taifa la Nupe na Nigeria kwa ujumla.

3497997

captcha