IQNA

Watu zaidi ya 100 wauawa katika hujuma ya kigaidi Mogadishu, Somalia

11:20 - December 29, 2019
Habari ID: 3472312
TEHRAN (IQNA) – Watu wasiopungua 100 wameuawa mapema Jumamosi na wengine wengi kujeruhiwa hujuma ya kigaidi katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu.

Mohamed Hussein mmoja wa maafisa wa polisi amewaambia waandishi wa habari kwamba, mlipuko wa gari lililotegewa bomu ulitokea katika kituo kimoja cha kukagua magari maarufu kama 'Ex Control' mjini Mogadishu.

Watu zaidi ya 100 wanaripotiwa kujeruhiwa wakiwemo watoto ambao tayari wamepelekwa hospitali. Idadi kubwa ya waliouawa walikuwa wanafunzi waliokuwa wakielekea katika chuo kikuu huku raia kadhaa wa Uturuki wakiwa miongoni mwa waliouawa.

Baadhi ya ripoti zinasema kuwa, iidadi ya watu waliouawa katika mlipuko huo inaweza kuuongezeka.

Hodan Ali mmoja wa afisa wa jiji la Mogadishu amesema kuwa, kuna uwezekano mkubwa wa idadi ya wahanga wa shambulio hilo la kigaidi kuongezeka kwani hali ya baadhi ya majeruhi ni mbaya sana.

Hakuna kundi ambalo limetangaza kutekekeleza shambulio hilo la kigaidi lakini wapiganaji wa kundi la kigaidi al-Shabab wamekuwa wakitekeleza mashambulizi ya  kigaidii mara kwa mara katika taifa hilo la pembe ya Afrika.

Rais Mohamed Abdullahi Farmaajo wa Somalia amelaani vikali hujuma hiyo ya kigaidi na kulaumu kundi la al Shaba kuwa ndilo ambale limetekeleza mauaji hayo.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amelaani vikali shambulio la kigaidi lililotokea jana Jumamosi katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu na kuua makumi ya watu.

António Guterres ametoa tamko rasmi usiku wa kuamkia leo na sambamba na kulaani shambulio hilo la kigaidi ameelezea kusikitishwa mno na kuwa pamoja kwake na serikali na wananchi wa Somalia katika wakati huu mgumu.

Jamhuri ya Kiislamu ya Iran zimelaani shambulizi hilo la kigaidi mjini Mogadishu. Katika taarifa, msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran Abbas Mousavi ametuma salamu za rambi rambi kwa familia za waliopoteza maisha katika shambulizi hilo ambalo limetajwa kuwa mbaya zaidi katika kipindi cha miaka miwili iliyopita Somalia.

Kundi la kigaidi la al Shabab lilianza hujuma zake nchini Somalia mwaka 2007 na limekuwa likiendesha ugaidi katika mji mkuu Mogadishu na maeneo mengine ya Somalia na pia katika nchi jirani ya Kenya. Magaidi hao walitumuliwa Mogadishu Agosti 2011 katika operesheni iliyofanywa vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Afrika AMISOM, lakini limekuwa likifanya mashamabulizi ya kuvizia mara kwa mara.

AMISOM ina askari wapatao 21,000 nchini Somalia ambao wanalinda amani katika nchi hiyo inayosumbuliwa na vita vya ndani kwa robo karne sasa.

Kundi la kigaidi la al Shabab, sawa na Boko Haram, Al Qaeda, ISIS ,  lina ufahamu usio sahihi na potovu kuhusu dini ya Kiislamu, limekuwa likitekeleza hujuma katika maeneo mbalimbali ya Somalia na nchini Kenya.

3867036

captcha