IQNA

Waislamu wa Marekani wako mstari wa mbele katika vita dhidi ya corona

11:30 - April 17, 2020
Habari ID: 3472672
TEHRAN (IQNA) - Kufuatia uhaba wa vifaa vya wauhudumu wa afya katika hospitali za Marekani, Waislamu wa nchi hiyo wameunda kundi la kujitolea katika kupambana na virusi vya Corona.

Kwa mujibu wa taarifa, kufuatia ongezeko la kila siku la maambukizi ya virusi vya Corona nchini humo sambamba na kushindwa serikali ya federali kutatua tatizo la uhaba wa vifaa vya kuwalinda wahudumu wa afya na pia kushtadi matatizo ya wananchi, kundi moja la Waislamu wa nchi hiyo limeamua kuwasaidia wahudumu wa afya kwa kuwapatia maski na nguo za kujikinga na maradhi ya Covid-19. Kwa mujibu wa ripoti hiyo, baadhi ya misaada hiyo ni hatua ya hivi karibuni ya 'Kituo cha Kiislamu cha Cincinnati' ya kujibu ombi la mtaalamu mmoja wa masuala ya akina mama na wazazi katika mji huo wa jimbo la Ohio, aliyetaka kutengenezwa maski za kiafya. Dr Maram Khabbaz, Mkuu wa Huduma za Kituo cha Kiislamu cha Cincinnati ameelezea suala hilo kwa kusema, hadi sasa Waislamu wa mji huo wamefanikiwa kugawa maski 1000 katika vituo vya afya.

Naye Janet Altino, Mkuu wa Mahusiano ya Umma wa Taasisi ya Afya ya TriHealth katika mji wa Cincinnati amesema kuwa, aina hiyo ya uungaji mkono wa jamii ya Waislamu kwa timu ya madaktari katika kipindi hiki cha mgogoro wa Corona, ni zawadi kubwa. Altino amesema: 'Tunashukuru kwa zawadi zote hizo na tunawashukuru wote waliochangia jambo hilo.' Katika wiki za hivi karibuni, majimbo tofauti ya Marekani yameshuhudia uhaba mkubwa wa vifaa vya afya na vya kujikinga madaktari na wauguzi zikiwemo maski na mavazi maalumu, hata hivyo serikali ya Rais Donald Trump imeendelea kuwataka wahudumu hao wa afya kutumia maski zilizokwishatumika kwa kuzifua.

3892066

Kishikizo: Corona marekani waislamu
captcha