IQNA

Iran yalalamika rasmi baada ya wakuu wa Ufaransa kumvunjia heshima Mtume Muhammad SAW

15:22 - October 27, 2020
Habari ID: 3473299
TEHRAN (IQNA- Balozi Mdogo wa Ufaransa mjini Tehran, Florent Aydalot, ameitwa katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kukabidhiwa malalamiko ya Iran kuhusu sisitizo la serikali ya Ufanrasa la kuwaunga mkono waliochapisha katuni zilizomvunjia heshima Mtume Muhammad SAW.

Kwa mujibu wa taarifa, katika mkutano na mwanadiplomasia huyo wa Ufaransa, Naibu Mkurugenzi wa Masuala ya Ulaya katika Wizara ya Mambo ya Iran, amelaani vikali vitendo visivyokubalika vya maafisa wa serikali ya Ufaransa ambao wameumiza hisia za mamillioni ya Waislamu Ulaya na kote duniani. Ameongeza kuwa, 'kitendo chochote cha kumtusi na kumvunjia heshima Mtume Mtukufu wa Uislamu (SAW), na pia kuvunjia heshima matukufu ya Kiislamu kinalaani vikali."

Ameongeza kuwa, inasikitisha kuona wanaochochea chuki dhidi ya Uislamu wanatumia kisingizio cha uhuru wa maoni.

Halikadhalika amesesma jibu lisilo la kimantiki la wakuu wa Ufaransa kwa vitendo vya wale wanaotumia mabavu kwa jina la Uislamu huandaa mazingira ya kuenea fikra hizo potovu ambazo haziendani na Uislamu.

 Naibu Mkurugenzi wa Masuala ya Ulaya katika Wizara ya Mambo ya Iran amesema Uislamu ni dini yenye kufunza kustahamiliana, mantiki, amani, utulivu na kupigania haki.

Kwa upande wake, Balozi Mdogo wa Ufaransa mjini Tehran amesema atafikisha malalamiko ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa serikali ya Ufaransa haraka iwezekanavyo.

Jarida la Ufaransa la Charlie Hebdo hivi karibuni lilichapisha tena katuni zenye kumvunjia heshima Mtume Muhammad SAW, kitendo ambacho kiliungwa mkono wazi wazi na Rais Emmanuel Macron wa nchi hiyo.

Kitendo hicho cha Macron kinaendelea kulalamikiwa vikali kote duniani ambapo kumeanzishwa wimbi la kususia bidhaa za Ufaransa.

3931465

captcha