Kwa mujibu wa taarifa, Amadou Tejan Won ameirejesha nishani hiyo kwa ubalozi wa Ufaransa mjini Dakar kama njia ya kulalamikia hatua ya wakuu wa Ufaransa kumvunjia heshima Mtume Muhammad SAW na kueneza chuki dhidi ya Uislamu. Tejan Won anasema awali wakati alipotunukiwa zawadi hiyo kubwa zaidi ya kiraia na kijeshi Ufaransa alihisi fahari kubwa.
“Niliitizama nishani hii kama nembo ya udugu, uhuru na usawa,” amesema na kuongeza kuwa, sasa hivyo hali imebadilika baada ya Mtume Muhammad SAW kuvunjiwa heshima Ufaransa na hivyo ameamua kuirejesha zawadi hiyo kwa ubalozi wa Ufaransa.
Matamshi ya Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa kwamba Uislamu uko kwenye mgogoro duniani kote na msimamo wake wa kuunga makono kitendo kiovu cha jarida la nchi hiyo la Charlie Hebdo cha kuchapisha vikatuni vya kumvunjia heshima Mtume Muhammad SAW kimeughadhibisha Ulimwengu wa Kiislamu.
Maandamano makubwa yamefanyika na yanaendelea kufanyika katika nchi mbalimbali kulaani msimamo huo wa Macron. Mbali na maandamano, zinaendeshwa kampeni pia za kususia bidhaa za Ufaransa na sasa kampeni hiyo pia imeenea katika sekta za utamaduni.