Sheikh Humam Hamoudi ameipongeza Idara ya Mahakama Iraq kwa kuchukua uamuzi wa kishujaa wa kutoa waranti wa kutaka Trump akamatwe.
Hivi karibuni Jaji maalumu wa mahakama ya Ar-Rasaafah ambayo ndiyo inayofuatilia mashtaka ya jinai iliyofanywa na Marekani dhidi ya Luteni Jenerali Qassem Soleimani, Kamanda wa Kikosi cha Quds cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC, na Abu Mahdi al Muhandis, Naibu wa Mkuu Taasisi ya Kujitolea ya Wananchi wa Iraq maarufu kwa jina la al Hashd al Shaabi, ndiye aliyetoa waranti wa kutiwa mbaroni rais wa Marekani, Donald Trump.
Kwa mujibu wa shirika rasmi la habari la Iraq WAA, hakimu maalum wa mahakama ya uchunguzi ya Ar-Rasaafah ametoa taarifa maalum na kutangaza kwamba, baada ya kukamilika mchakato wa kukusanya madai ya walalamikaji binafsi wa faili la kesi hiyo na pia uchunguzi wa awali, ametoa waranti wa kutiwa nguvuni Trump.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, uchunguzi utaendelea kufanywa kuwatambua wahusika wengine walioshiriki katika jinai ya mauaji hayo, wawe ni Wairaqi au raia wasio Wairaqi.
Wanajeshi magaidi wa Marekani waliwaua kidhulma shahid Soleimani na Abu Mahdi al Muhandis pamoja na wanamapambano wenzao wanane tarehe 3 Januari 2020 karibu na uwanja wa ndege wa Baghdad mji mkuu wa Iraq kwa amri wa rais wa Marekani, Donald Trump. Damu ya mashahidi hao itaendelea kuwaandama milele watenda jinai hao wakiongozwa na Donald Trump.
Luteni Jenerali Qassem Suleimani, ambaye mnamo usiku wa kuamkia tarehe 3 Januari 2020 alielekea Iraq kwa mwaliko rasmi wa viongozi wa nchi hiyo, aliuawa shahidi yeye na Abu Mahdi al Muhandis, Naibu Mkuu wa jeshi la kujitolea la wananchi wa Iraq Al Hashdu-Sha'abi pamoja na wanamuqawama wengine wanane katika shambulio la anga lililofanywa na jeshi la kigaidi la Marekani karibu na uwanja wa ndege wa Baghdad.
Kufuatia kuuawa shahidi makamanda hao wa muqawama, bunge la Iraq lilipitisha mpango unaowataka askari wa jeshi la kigaidi la Marekani waondoke nchini humo.