MAKKA (IQNA) – Afisa mwandamizi wa Saudia aliwapa ushauri Waislamu wanaolenga kutekeleza ibada ya Hija ndogo ya Umrah juu ya wakati gani ni mzuri wa ibada hiyo katika Msikiti Mkuu wa Makka au Masjid al-Haram.

Waziri wa Hija na Umra wa Saudia Tawfiq Al-Rabiah amesema katika msimu huu muda mzuri wa kuzuru Masjid al Haram kwa ajili ya Umrah ni asubuhi ni kuanzia saa moja na nusu hadi saa nne na nusu na kisha usiku kuanzia saa tano hadi saa nane.
Waziri huyo alisema katika taarifa yake kwenye akaunti yake ya X kwamba siku zisizo na watu wengi zaidi za kila wiki kwa ajili ya kutekeleza ibada ya Umrah ni Jumapili, Jumanne, Jumatano.
Ushauri wa waziri huyo ulikuja wakati Msikiti Mkuu wa Makka ukishuhudia wimbi kubwa la waumini wanaotekeleza ibada ya Umrah wakitokea duniani kote.
Al-Rabiah alisema kuwa Makka imekuwa ikishuhudia hali ya hewa ya kupendeza siku hizi na hii inawawezesha waumini kutekeleza ibada zao kwa urahisi na utulivu wa kiroho.
Umrah ni safari ya kwenda Makka ambayo Waislamu wanaweza kutekeleza wakati wowote wa mwaka, tofauti na Hija ambayo inaweza kufanywa tu katika siku za kwanza za mwezi wa Hijri wa Dhul Hajja.
3486148