IQNA

15:22 - August 21, 2026
Habari ID: 3482656

Rekodi mpya ya Waislamu waliopata nyadhifa za uongozi nchini Marekani mwaka 2026

IQNA – Baraza la Mahusiano ya Kiislamu nchini Marekani (CAIR) limetangaza kuwa Waislamu 255 wamechaguliwa kushika nyadhifa mbalimbali za umma katika majimbo 26 ya Marekani mwaka 2026, idadi kubwa zaidi kuwahi kurekodiwa. Viongozi hao wanahudumu katika karibu kila ngazi ya serikali, wakiwemo wajumbe wa Kongresi, maseneta na wawakilishi wa majimbo, majaji, meya, wajumbe wa mabaraza ya miji, bodi za shule na nafasi nyingine za mitaa.

w

Baraza la Mahusiano ya Kiislamu nchini Marekani (CAIR), shirika kubwa zaidi nchini humo la kutetea haki za kiraia na maslahi ya Waislamu, katika taarifa ya pamoja na kitengo chake cha CAIR Action, siku ya Alhamisi limetangaza kutolewa kwa “Orodha ya Viongozi Waislamu Waliochaguliwa ya Mwaka 2026.” Orodha hiyo imebainisha viongozi Waislamu 255 waliovunja rekodi, wanaohudumu katika majimbo 26 na katika karibu kila ngazi ya serikali.

Takwimu hizi mpya zinawakilisha hatua muhimu katika ushiriki wa kiraia na kisiasa wa Waislamu wa Marekani, na zinaonesha kuongezeka kwa uwepo wa watumishi wa umma Waislamu katika jamii mbalimbali nchini kote.

Kwa mujibu wa orodha hiyo, serikali za mitaa zinachukua sehemu kubwa zaidi ya uongozi wa Waislamu waliochaguliwa. Wajumbe 98 wa Kiislamu wanahudumu katika mabaraza ya mitaa, ikiwa ni asilimia 38.4 ya jumla ya viongozi Waislamu waliotambuliwa. Karibu robo ya viongozi hao wanahudumu katika nafasi zinazohusiana na elimu, ambapo viongozi 63 wa Kiislamu, sawa na asilimia 24.7 ya jumla ya kitaifa, wanahudumu katika sekta hiyo. Hii inafanya elimu kuwa eneo la pili kwa ukubwa la utumishi wa umma miongoni mwa Waislamu waliochaguliwa.

Mabunge ya majimbo yanachangia asilimia 18 ya viongozi Waislamu waliotambuliwa. Kwa pamoja, viongozi 46 wanahudumu kama wawakilishi wa majimbo au maseneta wa majimbo; kati yao wapo wawakilishi 32 wa majimbo, sawa na asilimia 12.5, na maseneta 14 wa majimbo, sawa na asilimia 5.5. Aidha, orodha hiyo imewatambua meya 11 Waislamu, ambao ni asilimia 4.3 ya viongozi wote Waislamu waliorekodiwa kitaifa.

Majaji 18 Waislamu pia wamejumuishwa katika orodha hiyo, wakichangia asilimia 7.1 ya viongozi wote waliotambuliwa na kuashiria uwepo wa Waislamu katika nyadhifa za mahakama zinazopatikana kwa uchaguzi. Wamarekani Waislamu wanne wanahudumu katika Baraza la Wawakilishi la Kongresi (Bunge) ya Marekani, ikiwa ni asilimia 1.6 ya jumla ya viongozi wote. Viongozi wengine 15 wanahudumu katika nafasi mbalimbali za kuchaguliwa, zikiwemo za utekelezaji wa sheria, manispaa, usafiri na sekta nyinginezo.

Kwa pamoja, wajumbe 98 wa mabaraza ya mitaa na viongozi 63 wa sekta ya elimu wanafikia 161 kati ya viongozi 255, sawa na asilimia 63.1 ya orodha nzima. Hali hiyo inaonesha kwamba karibu theluthi mbili ya viongozi Waislamu waliochaguliwa wanahudumu katika mabaraza ya mitaa au taasisi za elimu.

Orodha hiyo pia inaonesha uwakilishi mkubwa wa wanawake Waislamu katika nyadhifa za kuchaguliwa. Kati ya viongozi Waislamu 255 waliotambuliwa kote nchini, 110 ni wanawake, sawa na asilimia 43.1, huku 145 ni wanaume, sawa na asilimia 56.9. Hivyo, wanawake wanaunda zaidi ya wanne katika kila viongozi kumi Waislamu waliochaguliwa katika orodha ya mwaka 2026. Kiwango hiki kinazidi uwakilishi wa wanawake katika Kongresi ya Marekani, unaokadiriwa kuwa asilimia 28.2, na katika mabunge ya majimbo nchini humo, unaokadiriwa kuwa asilimia 33.6.

CAIR na CAIR Action zilisema kwamba baada ya kutangazwa kwa awali kwa mradi wa orodha hiyo, wanajamii Waislamu, viongozi wa mitaa, maafisa waliochaguliwa na matawi ya CAIR katika maeneo mbalimbali walitoa taarifa za ziada kuhusu viongozi Waislamu ambao hawakuwa wamejumuishwa katika hesabu ya kwanza. Kutokana na mwitikio huo wa jamii na uhakiki zaidi wa taarifa, idadi ya mwisho ya viongozi katika orodha iliongezeka kwa kiasi kikubwa ikilinganishwa na takwimu za awali.

Ongezeko hilo linaakisi, kwa upande mmoja, kuongezeka kwa idadi ya Waislamu wanaohudumu katika nyadhifa za umma, na kwa upande mwingine changamoto ya kuweka hesabu ya kitaifa iliyo kamili kuhusu viongozi Waislamu waliochaguliwa katika maelfu ya nafasi za shirikisho, majimbo, kaunti, manispaa, mahakama, bodi za shule na taasisi nyingine za mitaa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kitaifa wa CAIR, Nihad Awad, alisema idadi hiyo ya rekodi ni zaidi ya takwimu pekee, bali inaonesha jamii ya Waislamu wa Marekani inayozidi kuwa na ushiriki, yenye mpangilio na iliyojitolea kuitumikia nchi yake. Alisema kuwa kuanzia Kongresi na mabunge ya majimbo hadi mabaraza ya miji, bodi za shule na serikali za mitaa, Wamarekani Waislamu wanajitokeza kuwahudumia majirani zao na kuimarisha demokrasia ya nchi hiyo. Aliongeza kuwa, katika kipindi cha kuongezeka kwa matamshi dhidi ya Uislamu, watumishi hao wa umma wanatuma ujumbe kwamba Waislamu wa Marekani wataendelea kushiriki kwa uhuru na bila woga katika maisha ya kiraia ya taifa lao.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa CAIR Action, Bassim Elkarra, alisema idadi ya rekodi ya viongozi Waislamu waliotambuliwa katika orodha hiyo inaonesha kuimarika kwa nguvu ya kisiasa na ushiriki wa kiraia wa jamii za Waislamu kote nchini Marekani. Alisema ni jambo la kutia moyo kwamba baada ya kutangazwa kwa mradi huo, wanajamii kutoka maeneo mbalimbali walijitokeza kusaidia kutambua watumishi wengine Waislamu wa umma. Alisisitiza kuwa orodha hiyo si rekodi tu ya hali ya sasa, bali pia ni ukumbusho wa yale yanayowezekana wakati jamii zinapopiga kura, kujipanga, kugombea nafasi za uongozi na kushiriki katika kila ngazi ya demokrasia.

Orodha ya mwaka 2026 inajumuisha Wamarekani Waislamu wanaohudumu katika nyadhifa mbalimbali, zikiwemo za wajumbe wa Kongresi, maseneta wa majimbo, wawakilishi wa majimbo na wajumbe wa mabunge ya majimbo, majaji, meya, wajumbe wa mabaraza ya miji na kaunti, makamishna, wajumbe wa bodi za shule, makatibu na nafasi nyingine za kuchaguliwa. CAIR na CAIR Action zilisema orodha hiyo inalenga kuwa nyenzo kwa waandishi wa habari, watafiti, watunga sera, mashirika ya kiraia na jamii za Waislamu zinazotaka kufahamu kwa undani ukuaji na usambao wa uwakilishi wa Waislamu katika serikali ya Marekani.

3498729

captcha