IQNA

Utawala wa Aal Khalifa wavunja Taasisi ya Kiislamu ya Mashia Bahrain

10:54 - February 02, 2014
Habari ID: 1369535
Utawala wa Aal Khalifa nchini Bahrain umeanzisha wimbi jipya la kukabiliana na fikra huru, nara za kidini, harakati za jumuiya na taasisi huru za kidini nchini humo sanjari na vyombo vya sheria kutoa amri ya kuvunjwa Baraza la Maulamaa la nchi hiyo. Mahakama ya Bahrain siku ya Jumatano ilitoa amri ya kuvunjwa na kutaifishwa mali zote za baraza hilo.

Baraza la Maulamaa nchini Bahrain linahesabiwa kuwa taasisi kubwa zaidi ya wananchi na Waislamu wa Madhehebu ya Kishia nchini humo, na tokea ilipoanzishwa harakati na mwamko wa wananchi tarehe 14 Februari 2011, limekuwa na nafasi muhimu ya kuziongoza harakati za wananchi dhidi ya utawala wa kifalme wa Aal Khalifa. Hatua ya utawala wa Aal Khalifa ya kuzivunja  taasisi na jumuiya za Kiislamu nchini  Bahrain inaonyesha jinsi utawala huo ulivyoshindwa  kuishi  kwa maelewano na wananchi wa Bahrain, na kudhihirisha mwenendo na muamala wake wa kidikteta na ukiritimba pamoja na hofu na kiwewe kikubwa kilichoupata utawala huo wa kiimla juu ya harakati zozote za wananchi zinazofanyika katika kalibu ya taasisi za Kiislamu.
Nyendo za utawala wa kifalme wa Aal Khalifa zinaonyesha kuwa, utawala huo licha ya kukandamiza uhuru wa kisiasa wa wananchi unawazuilia pia wananchi haki zao nyingine za kimsingi kama vile uhuru wa kuendesha harakati zao za kidini. Utawala wa Bahrain ulikuwa na mikakati ya kuziweka taasisi na jumuiya zote za kidini na za kiraia kuwa chini ya udhibiti wake na kuzuia harakati za taasisi na jumuiya hizo. Hii ni katika hali ambayo, taasisi kadhaa za kisheria na hali kadhalika mawakili wa Bahrain wameonyesha radiamali zao kuhusiana na amri hii isiyokuwa ya kiadilifu na usawa ya vyombo vya sheria vya utawala wa Aal Khalifa. Taasisi ya Haki za Binadamu ya Bahrain imetangaza kuwa, kuvunjwa Baraza la Maulamaa ni dhulma kubwa na inayochukiza mno.
Wadadisi wa masuala ya kisiasa wanaamini  kuwa, harakati za Baraza la Maulamaa wa Kiislamu  zilikuwa na shabaha ya kuinyanyua nafasi ya muqawama wa wananchi wa Bahrain, na kwamba hatua ya  kuvunjwa baraza hilo bila shaka itaziumiza nyoyo  za wananchi na hatimaye kuvurugika  mwenendo wa  mazungumzo ya kitaifa. Utawala wa Aal Khalifa uliyaita makundi ya upinzani kwenye mazungumzo ya kitaifa ili kuvuta muda, na wachambuzi wa mambo wanasema kuwa, utawala huo umefanya hivyo ili kupunguza  malalamiko na mashinikizo ya wananchi  kwani hauna nia njema na ya dhati ya kufanya mazungumzo na wapinzani.  Vitendo  dhidi ya dini  tukufu ya Kiislamu na vile vya uharibifu vinavyofanywa na utawala huo wa kifalme vya kubomoa makumi ya Misikiti tangu wakati zilipoanza harakati za wananchi wa Bahrain, vimewafanya walimwengu na hasa Waislamu wabaini  uhakika huu kwamba utawala huo una ajenda za kuyavunjia heshima matukufu ya Kiislamu kwa kuvamia maeneo na taasisi za kidini.
Utawala wa Aal Khalifa kila mara unakabiliana na mafundisho ya Kiislamu yanayokabiliana na sera za madola ya kibeberu, mafundisho ambayo yanaonekana kuwa ni kikwazo cha kuendelea kubakia madarakani utawala huo wa kidikteta. Kwa upande huo, utawala wa Aal Khalifa  umeweka azma ya kulenga  itikadi za  Kiislamu za wananchi wa Bahrain na kuwalazimisha wananchi wazikubali siasa zake za  kibeberu. Utawala huo unazibana harakati na shughuli za kidini, suala ambalo litawahamasisha zaidi wananchi waendelee kukabiliana na utawala huo usiokuwa wa kidemokrasia na kuandaa mazingira ya kuwepo utawala wa wananchi utakaofuata misingi ya kidini.
1368508

captcha