Katika tukio la kwanza, gaidi aliyekuwa amesheheni bomu amejilipua ndani ya Msikiti wa Badr kusini mwa Sana'a wakati wa sala ya Ijumaa. Wakati watu wakijaribu kutoka nje ya msikiti, gaidi mwingine aliyekuwa amesimama mlangoni alijilipua na hivyo kuongeza idadi ya waliopoteza maisha.
Hujuma ya pili ilijiri katika Msikiti wa al-Hashoosh kaskazini mwa Sana'a ambapo gaidi aliyekuwa amesheheni mabomu alijilipua ndani ya misikiti.
Walioshuhudia wanasema bomu hilo lilikuwa na guvu kubwa na kwamba vichwa, miguu na mikono ya waliofariki ilikuwa imetapakaa katika sakafu ya msikiti. Shuhuda mmoja aliyetambuliwa kama Mohammad al-Ansi amesema: 'Damu hapa inatiririka kama mto."
Misikiti miwili iliyohujumiwa ya al-Hashoosh na Badr ni ya Waislamu wa Madhehebu ya Shia na imedokezwa kuwa kati ya waliouawa katika hujuma hiyo ni Sheikh al-Murtadha bin Zaid al-Mahtouri kiongozi mwandamizi wa kidini katika Harakati ya Ansarullah. Sheikh al-Mahtouri alikuwa Mkuu wa Taasisi ya Utamaduni ya Badr na alikuwa kati ya wanazuoni wa ngazi za juu katika Fiqhi ya Zaydi nchini Yemen. Kundi la kigaidi la Daesh (ISIL) limedai kuhusika na hujuma hizo za kigaidi dhidi ya misikiti mjini Sana'a.../mh